1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mzozo kati ya nchi za Ukraine na Urusi waitikisa dunia

25 Februari 2022

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky ametia saini agizo la kuwataka wananchi wake wajiandae kwa ajili ya ulinzi. Agizo hilo litatekelezwa kwa muda wa miezi mitatu.

https://p.dw.com/p/47ZE0
Ukraine Konflikt | Präsident Volodymyr Zelenskyy
Picha: Ukrainian Presidency / Handout /AA/picture alliance

Kwa mujibu wa taarifa raia pamoja na jeshi la akiba wanaandikishwa kwa ajili ya kuilinda nchi yao kutokana na uvamizi wa Urusi.  Wanaume wenye umri wa kuanzia miaka 18 hadi 60 sasa hawaruhusiwi kuondoka nchini. Wakati huo huo majeshi ya Urusi tayari yameshaingia nchini Ukraine na yako mbele ya mji mkuu wa nchi hiyo Kiev.

Afisa mmoja wa ujasusi wa nchi ya magharibi ameliambia shirika la habari la AFP kuwa Urusi sasa inaidhibiti anga ya Ukraine. Nchi hiyo sasa haina tena jeshi la anga la kuilinda.Kwa mujibu wa  taarifa ya afisa huyo wa ujasusi, Urusi itaingiza idadi kubwa ya askari karibu na mji mkuu katika muda wa saa chache zijazo.Taarifa zaidi zinasema majeshi ya Urusi yameshauteka uwanja wa ndege wa jeshi la Ukraine pamoja na kinu cha nyuklia cha Chernobil kilichopatwa na ajali mnamo mwaka 1986.

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa
Baraza la Usalama la Umoja wa MataifaPicha: Timothy A. Clary/AFP

Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa litapiga kura leo Ijumaa juu ya azimio ambalo litalaani uvamizi wa kijeshi wa Urusi dhidi ya Ukraine. Baraza hilo la Usalama pia kwa kauli Kali litaitaka ufrusi kusirtisha uvamizi dhidi ya Ukraine na kuwaondoa wanajeshi wake mara moja. Azimio hilo lilipitishwa haraka hapo jana katika Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lenye wanachama 193 wasio na kura ya turufu. Dhamira ya Baraza Kuu la Umoja wa Matafa ni kudumisha uhuru, umoja, na uadilifu wa kuheshimu maeneo ya Ukraine yaliyo ndani ya mipaka yake inayotambulika kimataifa.

Soma: Urusi yaendeleza uvamizi Ukraine katika "siku ya giza" Ulaya

Wakati huo huo kundi la kwanza la wakimbizi kutoka Ukraine limewasili nchini Poland ambayo ni nchi mwanachama wa Umoja wa Ulaya. Wakimbizi hao wameingi anchini humo kwa njia za barabara na reli.

Rais wa Marekani Joe Biden
Rais wa Marekani Joe BidenPicha: Brendan Smialowski/AFP

Rais wa Marekani Joe Biden ametangaza vikwazo vipya dhidi ya Urusi baada ya nchi hiyo kuivamia Ukraine. Vikwazo hivyo vinalenga benki nne za Urusi, matajiri wakubwa wa nchi hiyo pamoja na sekta ya teknolojia. Biden ameeleza kuwa Marekani na washirika wake wataiwekea Urusi vizuizi na kudhibiti mauzo ya nje kwa nchi hiyo. Vile vile Marekani imesema itapeleka majeshi ya ziada nchini Ujerumani kuimarisha vikosi vya jumuiya ya kujihami ya NATO baada ya Urusi kuvamia Ukraine, ambayo si mwanachama wa jumuiya hiyo ya kijeshi.

Angalia:

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema chombo hicho cha ulimwengu kimeandaa dola milioni 20 kwa ajili msaada wa dharura kwa watu wa Ukraine. Guterres amemtaka rais wa Urusi asitishe mara moja operesheni ya kijeshi na awarejeshe wanajeshi wake nchini Urusi.

Rais wa Urusi Vladimir Putin amesema mashambulio hayo yamekusudiwa ili kuwalinda raia wa mashariki mwa Ukraine, eneo ambalo waasi wanaoiunga mkono Urusi wamekuwa wakipambana na serikali ya Ukraine kwa takriban miaka minane.

Mbele: Rais wa Urusi Vladimir Putin. Nyuma: Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky.
Mbele: Rais wa Urusi Vladimir Putin. Nyuma: Rais wa Ukraine Volodymyr Zelensky.Picha: Mikhail Metzel/TASS/dpa/picture alliance

Rais wa halmashauri ya Ulaya Ursula Von der Leyen amesema viongozi wa Jumuiya hiyo ya Umoja wa Ulaya wamekubaliana juu ya hatua za kuiwekea Urusi vikwazo. Vikwazo hivyo vitazilenga sekta za benki na makampuni muhimu yanayomilikiwa na serikali ya Urusi.

Soma:Putin asema maslahi ya Urusi hayajadiliwi katikati mwa mzozo wa Ukraine

Akiwahutubia viongozi wenzake wa nchi zilizoendelea kiviwanda za kundi la G-7 mjini Brussels, Waziri Mkuu wa Italia Mario Draghi ametahadharisha kuwa mgogoro wa Ukraine unaweza kuchukua muda mrefu, na hivyo amewataka wanachama hao G7 kujiandaa. Draghi amesema Italia inaungana kikamilifu na Ujerumani, Ufaransa na nchi nyingine za Umoja wa Ulaya kuhusu kuiwekea Urusi vikwazo.

Vyanzo:AFP/AP/RTRE/https://p.dw.com/p/47Z1t