1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

Kiongozi wa maandamano Bangladesh ahofia usalama

Hawa Bihoga | Saumu Njama
22 Julai 2024

Kiongozi wa maandamano ya wanafunzi nchini Bangladesh Nahid Islam akiwa katika kitanda hospitalini baada ya kupigwa, kujeruhiwa na kutishwa na watu waliojitambulisha kuwa polisi amesema anahofia juu ya usalama wake.

https://p.dw.com/p/4ib2x
Bangladesh | jeshi likilinda doria baada ya maandamano ya wanafunzi kupigwa marufuku.
Jeshi la Bangladeshi likiwa mtaani kuzuia waandamanaji wanaopinga upendeleo wa nafasi za ajira.Picha: Mohammad Ponir Hossain/REUTERS

 

Mhitimu huyo wa masuala ya sosholojia mwenye umri wa miaka 26 anaeongoza vuguvugu la maandamano ya wanafunzi dhidi ya upendeleo wa nafasi za ajira zinazotafutwa serikalini na kuzusha maandamano makubwa juma lililopita, amesema maisha yake yapo hatarini.

Nahid pamoja na kundi lake ambao waliamua kusitisha maandamano kwa saa arobaini na nane siku ya Jumatatu aliongeza kwamba hakupendelea kuona kumwagika kwa damu zaidi, mauaji na hata uharibifu wa mali pia.

Tabia yake ya kusema kwa upole -- isiyo ya kawaida miongoni mwa viongozi wa wanafunzi wa Bangladeshi -- inapingana na  uamuzi wake wa dhati wa kusitisha maandamano kwa saa 48.

Maandamano hayo dhidi ya upendeleo, ambao wakosoaji wanasema hutumiwa kuwanufaisha wafuasi wa chama tawala cha Awami League, yanatajwa kuwa ni mabaya zaidi na wataalamu wanasema yalionesha hali halisi ya ombwe la ajira linalosababishwa na wasimamiaji wa mfumo.

Akiwa amevalia bendera ya taifa  Nahid aliwahamasisha waandamanaji vijana ambao walikaririwa wakiimba "Sifa! Sifa! Sifa."

Hata hivyo siku ya Jumamosi asubuhi watu waliojitambulisha kama askari polisi walimvamia kwa kuvunja mlango wa nyumba alimokuwa akiishi baada yake yeye kukaidi kutoka nje kutokana na amri ya kutotoka nje iliyotolewa na serikali.

Soma pia:Bangladesh yafutilia mbali vipengee vya upendeleo vya kazi

Alijaribu kuwakimbia watu hao lakini hakufanikiwa, kiongozi huyo wa vuguvugu la maandamano ameliambia shirika la habari la AFP kwamba watu hao walimkamata kwa nguvu na kuondoka nae.

"Watu watano walinishusha kwa nguvu na kunipeleka kwenye gari lao. Nilifunikwa macho na kufungwa pingu,"

"Kwa nini tunafanya hivi, lengo letu ni nini, kwa nini hatukusitisha maandamano, ni nani alikuwa nyuma ya vuguvugu hili," Nahid alisema hayo yalikuwa ni miongoni mwa maswali alioulizwa huku akiwa kwenye mateso makali chini ya watu waliojitambulisha askari.

"Hawakufurahishwa na majibu yangu na ndipo wakati fulani wakaanza kunipiga, walinipiga na kitu kama chuma na wakati fulani nilipoteza fahamu."

Aliongeza kuwa alipopata fahamu alijikuta yupo  kando ya barabara mashariki mwa mji mkuu Dhaka mapema Jumapili asubuhi na kufikishwa hospitali.

Nahid hakupata ajira tangu alipohitimu chuo kikuu cha Dhala lakini amekuwa akijihusisha siasa za wanafunzi na kuendeleza vuguvugu la maandamano dhidi ya fursa za ajira mnamo 2018.

Maandamano yageuka ghasia mbaya zaidi

Maandamano ya wanafunzi kote Bangladesh ya kupinga upendeleo katika kuajiri wafanyakazi kwenye sekta ya umma yaligeuka na kuwa ghasia mbaya zaidi wiki hii, ambazo zimedhihirisha changamoto za ukosefu wa ajira katika taifa hilo la saba kwa wingi wa watu duniani. 

Bangladeshi | Wanafunzi wakipinga upendeleo wa ajira.
Wanafunzi wakiandamana juu ya upendeleo wa ajira unaofanyika serikaliniPicha: Muhib Hasan

Waandamanaji wanataka mageuzi ya mfumo wa upendeleo ambao unahifadhi zaidi ya nusu ya kazi zinazotafutwa sana serikalini kwa makundi fulani, ikiwa ni pamoja na wanawake, walemavu na kizazi cha maveterani wa Vita vya Uhuru vya 1971.

Mahakama Kuu ya Bangladesh mwezi uliopita ilirejesha mgawo huo, ambayo serikali iliufuta mwaka 2018.

Makali ya upinzani wa wanafunzi, ambao umesababisha vifo vya takriban watu 39 katika mapigano kati ya waandamanaji na wafuasi wa serikali, ni sehemu ya uchumi unaoyumba ambao umeshindwa kutengeneza ajira za kutosha kwa vijana wanaounda zaidi ya robo ya wakazi.

Rashed Al Mahmud Titumir, profesa wa masomo ya maendeleo katika Chuo Kikuu cha Dhaka na mwenyekiti wa taasisi ya utafiti wa kiuchumi amesema muktadha wa vuguvugu la mageuzi ya upendeleo unahusu usalama, au ukosefu wa usalama unaoendelea kuhusu ajira na mapato, miongoni mwa vijana.

Soma pia:Jeshi la Bangladesh laingia mtaani kuwadhibiti waandamanaji

Kulingana na takwimu za rasmi za kitaifa, Takriban raia mmoja kati ya watano wa Bangladeshi kati ya umri wa miaka 15 hadi 24 hawako kazini wala darasani.

Wahitimu wa vyuo vikuu wanakabiliwa na viwango vya juu vya ukosefu wa ajira kuliko wenzao wasio na elimu nzuri, na wahitimu wapatao 650,000 ni miongoni mwao zaidi ya vijana milioni 2 wanaoingia kwenye soko la ajira kila mwaka.

Maktaba za vyuo vikuu zimejaa wahitimu wachanga kujiandaa kwa mtihani wa utumishi wa umma, kupambania uhaba wa kazi za serikali zinazoahidi usalama wa kazi, mapato mazuri na heshima.

Hali ya ukosefu wa ajira Bangladesh

Kulingana na vyombo vya habari vya ndani, mtihani wa kazi za umma wa mwaka jana ulifanywa na watahiniwa 346,000 kushindania nafasi 3,300 pekee.

Aidha ajira za kazi za mikono kama vile utengenezaji bidhaa, uchimbaji madini, ujenzi na utengenezaji wa magari pia zimekuwa ngumu kupatikana, hata sekta ya nguo ambayo Bangladesh ni muajiri mkubwa.

Bangladesh |  Watu wakiwa kwenye msururu.
Wafanyakazi wa kigeni wakipanga mastari kukata tiketi baada za ndege baada ya maandamano ya kupinga ajira kushika kasi Bangladesh.Picha: Mohammad Ponir Hossain/REUTERS

Idadi kubwa ya wanawake wamejiunga na maandamano hayo, na wanafunzi wengi wa kike walijeruhiwa wakati maandamano hayo yalipogeuka kuwa ghasia.

Wanawake wanakabiliwa na changamoto zaidi katika kupata elimu na ajira, na tafiti za serikali zikionyesha asilimia 27 ya wanawake na wasichana wenye umri wa miaka 15 hadi 24 wanakosa kazi na elimu, ikilinganishwa na asilimia 10 ya vijana. Hali ambayo Titumir anasema inawaacha wanawake katika hatari zaidi ya unyanyasaji wa nyumbani na umaskini.

Suala kuu linaloibua mzozo ni juu ya asilimia 30 ya kazi za utumishi wa umma zilizotengwa kwa ajili ya watoto na wajukuu wa "wapiganaji wa uhuru" waliopigana katika vita vya ukombozi vya Bangladesh

kutoka kwa Pakistani. Waandamanaji wanasema kuwa kazi chache zinapaswa kutengwa kwa ajili ya wajukuu wa wapiganaji.

Soma pia:Idadi ya walouwawa katika machafuko Bangladesh yafikia 105

Farhana Manik Muna, mratibu wa maandamano katika jiji la Narayanganj, alisema wanaharakati wanataka serikali iunde tume ya kupendekeza mageuzi ya mfumo wa upendeleo.

Farhana ameongeza kusema kwamba hawatoi wito wa kufutwa kwa jumla nafasi zilizotengwa kwa watu maalum, badala yake tunataka njia inayofaa kusaidia vikundi visivyo na uwezo wakiwemo wanachama wa jumuiya ndogo za Wenyeji na watu wa Bangladesh wenye ulemavu.

Waandamanaji wanadai watu zaidi waajiriwe kwa kuzingatia sifa. Huku wanaharakati wengine wakisema Bangladesh inahitaji zaidi mkakati wa kina wa kuboresha soko la ajira.

Ukosefu wa ajira umelazimisha mamilioni ya watu wa kipato cha chini na wasio na ujuzi kutafuta kazi nje ya nchi ili kutuma nyumbani fedha, wakati Bangladesh ikikabiliwa na wataalamu kutafuta ajira katika nchi zenye mapato ya juu.

Watu Milioni 800 wanaishi kwenye umasikini uliokithiri