1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Waziri Mkuu wa zamani wa Mali afariki dunia akiwa kizuizini

Saleh Mwanamilongo
22 Machi 2022

Nchini Mali,hisia bado ni kali baada ya kifo cha Waziri Mkuu wa zamani Soumeylou Boubèye Maïga mjini Bamako. Rais wa Niger alikiita kifo hicho kuwa ni mauaji. 

https://p.dw.com/p/48pOz
Waziri Mkuu wa zamani wa Mali Soumeylou Boubèye Maiga amefariki akiwa na umri wa miaka 68
Waziri Mkuu wa zamani wa Mali Soumeylou Boubèye Maiga amefariki akiwa na umri wa miaka 68Picha: MICHELE CATTANI/AFP

Waziri Mkuu huyo wa zamani wa Mali, mwenye umri wa miaka 68, alikamatwa na kisha kuwekwa chini ya waranti ya kukamatwa Agosti mwaka jana, kama sehemu ya uchunguzi wa kupambana na rushwa, unaohusishwa hasa na kandarasi za zana za kijeshi wakati alipokuwa Waziri Mkuu.

Hali ya afya yake ilikuwa imezorota sana kutokana na mazingira ya kuzuiliwa kwake. Soumelylou Boubeye Maiga, alikuwa amelazwa hospitalini takriban miezi mitatu iliyopita, lakini kuhamishwa kwake kwa matibabu, licha ya mapendekezo la madaktari wake, halikuweza kuruhusiwa na mamlaka ya mpito.

Macron atarajiwa kuwaondoa wanajeshi wake Mali

Familia imekataa uchunguzi wa maiti

Abdina Karembe, mwenyekiti wa tawi la vijana la chama cha CFP, cha waziri mkuu huyo wa zamani amesema kiongozi wao amefariki kutokana na huduma mbovu ya matibabu.

''Aliteswa sana, na hatutaki tena kuutesa mwili wake kwa sababu viongozi wameomba kuweko na uchunguzi wa maiti ilikufahamu chanzo cha kifo chake. Familia imeamua kuwa haiitaji uchunguzi huo. Mazingira ya kushikiliwa kwake yalikuwa magumu kila mtu amefahamu hilo.''

Serikali ilitoa taarifa baadaye Jumatatu ikitangaza kwamba Maiga alikufa baada ya ugonjwa wa muda mrefu na kuwasilisha rambirambi kwa familia.

Mali na Mauritania zavutana

''Anapaswa kufunguliwa mashtaka kwa hili''

Rais wa Niger Mohamed Bazoum akiwa na Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron
Rais wa Niger Mohamed Bazoum akiwa na Rais wa Ufaransa Emmanuel MacronPicha: Francois Mori/AP Photo/picture alliance

Kwenye mtandao wake wa Twitter, Rais wa Niger Mohamed Bazoum alisema kunyimwa huduma ya matibabu nje ya nchi kwa Maiga ilikuwa sawa na mauaji. Huku akilinganisha kifo cha Maiga sawa na kile cha Rais Modibo Keita mwaka 1977 ambaye pia alifariki akiwa gerezani. Ujumbe huo umekosolewa vikali na utawala wa Bamako.

Aboubacar Sidick Fomba, mjumbe wa Baraza la Kitaifa la Mpito la Mali (CNT), amesema Rais wa Niger Mohamed Bazoum ni kibaraka cha Wafaransa na ambaye anastahili kufunguliwa mashtaka kwa maoni yake hayo.

''Tunatoa wito kwa mamlaka ya kipindi cha mpito kuchukua hatua za kisheria dhidi ya Rais wa Niger Mohamed Bazoum. Kwa sababu akizungumzia mauaji, hiyo inamaanisha kwamba ana uthibitisho. Na, tunatarajia atuletee ushahidi huo. Anapaswa kufunguliwa mashtaka kwa hili."

Maiga, aliyekuwa waziri wa ulinzi, aliteuliwa kuwa waziri mkuu mnamo 2017 na kujiuzulu miaka miwili baadaye, wiki nne baada ya mauaji ya wafugaji wapatao 160 wa kabila la Fulani yaliyofanywa na kikundi wanamgambo waliojiita walinda haki.