1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUrusi

Vikwazo vya Umoja wa Ulaya kwa Urusi vinaleta tija?

22 Februari 2024

Umoja wa Ulaya umetangaza vikwazo vipya dhidi ya Urusi, wakati ambapo mapema mwezi huu nchi hiyo ilitoa taarifa juu ya kustawi zaidi kwa uchumi wake. Pana mashaka na maswali iwapo je, vikwazo hivyo vitaleta tija?

https://p.dw.com/p/4cl2E
Brüssel Europaparlament Plenarsaal
Bunge la Umoja wa UlayaPicha: Dwi Anoraganingrum/Future Image/IMAGO

Umoja wa Ulaya umeongeza majina ya watu na kampuni zipatazo 200 kwenye orodha ya vikwazo dhidi ya Urusi kuelekea mwaka wa pili tangu Urusi ifanye uvamizi nchini Ukraine.

Mabalozi wa nchi za Umoja wa Ulaya wamekubaliana kuongeza majina hayo ya watu na kampuni juu ya takriban majina 2000 ya hapo awali. Hiyo ni duru ya 13 ya vikwazo dhidi ya Urusi.

Hata hivyo wachunguzi ikiwa pamoja na wa nchini Ukraine wana mashaka iwapo vikwazo hivyo vya nyongeza vitaweza kuiathiri Urusi.?

Wakati Umoja wa Ulaya unakabiliwa na maswali kadhaa juu ya wigo na ufanisi wa mkakati wake wa vikwazo, mkuu wa sera za nje wa Umoja huo Josep Borrell, alikuwa miongoni mwa wanadiplomasia wa jumuiya hiyo walioshangilia juu ya kuchukuliwa hatua hiyo nyingine dhidi ya Urusi.

Borrell ameeleza kuwa Umoja wa Ulaya umechukua hatua nyingine inayozilenga taasisi zinazovikwepa vikwazo  vilivyokwishawekwa na Umoja huo.Maelezo ya kina yatatolewa baada ya vikwazo kuidhinishwa rasmi. 

Soma pia:Urusi yakataa uchunguzi wa kimataifa kuhusu kifo cha Navalny

Ubelgiji ambayo sasa ni rais wa zamu wa baraza la Umoja wa Ulaya imesema itafaa maelezo hayo yatolewe hapo siku ya Jumamosi ambapo unatimia mwaka wa pili tangu Urusi ilipoivamia Ukraine.

Gazeti la Financial Times limeripoti kwamba kampuni zitakazoathirika na vikwazo hivyo vipya ni za China, India na Sri Lanka. Kampuni nyingine ni za Uturuki,Thailand,Serbia na Kazakhstan.

Pamoja na kuziorodhesha taasisi za Urusi, lengo  la vikwazo hivyo vipya ni kuzishinikiza nchi zinazoisaidia Urusi kukwepa vikwazo vilivyokwishawekwa.

EU yaoneza mbinyo kwa vikwazo zaidi kwa Urusi

Bila ya kutaja majina ya nchi au kampuni, rais wa Umoja wa Ulaya, Ursula von der Leyen, amesema hatua mpya  zilizochukuliwa zitaendeleza shinikizo dhidi ya Urusi na hivyo kuzizibia njia ya kupata ndege za droni. Amesema inapasa  kuendelea kuipunguzia Urusi uwezo wake wa kijeshi.

Rais wa Umoja wa Ulaya, Ursula von der Leyen
Rais wa Umoja wa Ulaya, Ursula von der LeyenPicha: FREDERICK FLORIN/AFP

Hata hivyo mjumbe wa Ukraine kwenye Umoja wa Ulaya amesema hatua hizo mpya dhidi ya Urusi haziendi mbali bali ni kama ishara kwamba zinapitishwa muda mfupi tu kabla ya siku ya kutimia mwaka wa pili tangu Ukraine ivamiwe.

Vikwazo vya hapo awali vilizilenga sekta muhimu za Urusi za mauzo ya nje, ikiwa pamoja na mafuta ghafi, makaa ya        mawe, dhahabu na almasi.

Lakini miaka miwili baada ya vikwazo hivyo kuwekwa, inaonekana kana kwamba Umoja wa Ulaya umeishiwa baruti nene za vikwazo. Aidha ni vigumu kwa wanachama wote 27 kukubaliana. Vikwazo katika sekta ya nishati ni vigumu kisiasa. 

Soma pia:Watu 23,000 wamepotea kufuatia uvamizi wa Urusi, Ukraine

Kutokana na nchi kadhaa za Umoja wa Ulaya kuwa tegemezi kwa Urusi kwa ajili ya mahitaji ya gesi, mauzo ya bidhaa hiyo kwa nchi za Umoja wa Ulaya yaliongezeka katika miezi sita ya kwanza mnamo mwaka uliopita. Taarifa hiyo inatokana na tathmini iliyofanywa na jopo la kampeni, maarufu kwa jina la Global Witness.

Baadhi ya wanadiplomasia wa Umoja wa Ulaya wamesema hatua hizo mpya hazitoshelezi hasa baada ya kifo cha  mpinzani mkubwa nchini Urusi, Alexei Navalny.

Licha ya vikwazo vya Umoja wa Ulaya uchumi wa Urusi umekuwa unastawi kwa uthabiti. Pato jumla la Urusi lilirejea katika kiwango cha asilimia 3.6 mwaka uliopita. 
 

Ujerumani: Hatutaiacha Ukraine kwenye vita peke yake