1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Umoja wa Ulaya wahimiza uhuru wa umma Senegal

12 Februari 2024

Umoja wa Ulaya umeitaka mamlaka nchini Senegal kutoa hakikisho la msingi wa uhuru wa umma baada ya machafuko, yaliyosababishwa na kuahirishwa kwa uchaguzi wa rais, kugharimu maisha ya watu watatu.

https://p.dw.com/p/4cH9V
Machafuko Senegal
Waandamanaji wakionesha ishara baada ya polisi kuwarushia vitoa machozi nje ya Mkutano Mkuu wa Plateau, Dakar Februari 5, 2024.Picha: John Wessels/AFP

Msemaji wa ofisi ya sera za mambo ya nje na usalama ya umoja huo, Nabila Massrali, kupita ukurasa wa X zamani Twitter ameandika "Umoja wa Ulaya unatoa salamu zake za pole kwa jamaa za waliouwawa na kutoa wito kwa mamlaka kuhakikisha upatikanaji wa msingi wa uhuru."

Katika hatua nyingine idadi ya waliokufa katika kipindi hiki ambacho taifa hilo limegubikwa na maandamano yaliosababishwa na kuahirishwa kwa uchaguzi wa rais hadi Desemba imeongezeka na kufikia watu watatu.

Wasiwasi katika eneo la Afrika Magharibi lenye tishio la mapinduzi

Maandamano ya Senegal katika mitaa ya Dakar
Maandamano ya Senegal katika mitaa ya Dakar. Mwandamanaji akionesha ishara huku wengine wakipiga picha wakati wa makabiliano na polisi wa kutuliza ghasia.Picha: Zohra Bensemra/REUTERS

Idadi hiyo inaelezwa katika kipindi ambacho wasiwasi ukiongezeka katika taifa hilo linaloatazamwa kama mfano wa kidemokrasia katika eneo la Afrika Magharibi ambalo limekumbwa na tisho la matukio ya mapinduzi.

Tangazo la kucheleweshwa kwa uchaguzi, ikiwa ni takriban majuma matatu kabla ya ule uliopangwakufanyika Februari. 25 umezusha vurugu za makabilino ya polisi na raia mjini Dakar, na maeneo mengine ikiwa ni nyongeza ya wimbi la maandamano ambayo inawafanya wengi wawe na hofu ya kuvurugika kwa amani katika kipindi kirefu.

Msimamo mwa Rais Macky Sall kwa kubadili siku ya uchaguzi

Vurugu katika viunga vya Dakar, Senegal
Waandamanaji wanakimbia huku bomu la machozi likitua karibu yao wakati wa makabiliano na polisi huko Dakar Februari 9, 2024.Picha: GUY PETERSON/AFP

Rais Macky Sall wa Senegal tayari amekwisha sema kuwa kuchelewesha ni muhimu kwa sababu migogoro ya uchaguzi ilitishia uhakika wa zoezi la uchaguzi, lakini baadhi ya wabunge wa upinzani wamekosoa hatua hiyo na kusema kuwa ni "mapinduzi ya kikatiba."

Wakati malalamiko ya umma yakiongezeka, Jumuiya ya Kiuchumi ya Mataifa ya Afrika Magharibi, ECOWAS na mataifa ya kigeni yamemtaka Rais Sall kurejea katika misingi ya kawaida ya uchaguzi.

Utata wa idadi ya vifo tangu mwanzo wa maandamano Senegal

Kwa mujibu wa Cartogra Senegal Huru (CFS), Jukwaa la mashirika ya kiraia, lenye kufuatilia athari za maandamano hayo, kifo cha kijana mmoja kati ya maandamano yaliyoripotiwa katika eneo la kusini mwa jiji la Zinguinchor Jumamosi kiliongeza idadi ya watu waliuwawa tangu Ijumaa kufikia watatu.

Ndiame Diop, meneja wa hospitali ya Ziguinchor, aliliambia shirika la habari la Uingereza, Reuters "Tulijaribu kumuokoa alipofika hospitali na kwa bahati mbaya alifariki akiwa katika chumba cha wagonjwa mahututi." Aliongoza kusema ilikuwa ngumu kwa mara moja kubaini kiini cha kifo chake pasipo uchuguzi wa maiti.

Soma zaidi:Mwanafunzi mmoja auawa katika maandamano nchini Senegal

Msemaji wa wizara ya mambo ya ndani ya Senegal haikuweza kupatikana kuelezea taarifa za kina kuhusu vifo hivyo. Wizara hiyo hadi sasa imethibitisha kifo kimoja tu cha mwanafunzi katika mji wa kaskazini wa Saint-Louis kilichotokea Ijumaa.

Wabunge wa upinzani na wagombea urais wanaokataa kuahirishwa kwa tarehe ya uchaguzi, wamewasilisha malalamiko ya  kisheria na kusema watamkataa na kumtambua Sall, kama rais baada ya mamlaka yake ya awali kumalizika mapema Aprili. Lakini nini hasa kitakachotokea siku zijazo, bado hakijawa wazi.

Chanzo: AFP/RTR