1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Uganda kuchapua ukuaji uchumi katika mwaka ujao wa kifedha

14 Juni 2022

Bajeti ya Uganda ya mwaka ujao wa kifedha imesomwa bungeni ikilenga kuchapua ukuaji wa kiuchumi kwa kuwawezesha raia zaidi kushiriki uchumi wa kifedha huku serikali ikitangaza kutoongeza ushuru kwa bidhaa msingi.

https://p.dw.com/p/4ChTM
Uganda Kampala Kinderarbeit
Picha: DW/Alex Gitta

Kulingana na waziri wa fedha wa Uganda Matia Kasaija, bajeti ya mwaka ujao wa kifedha imepangwa kuwaletea nafuu raia waweze kuimudu hali ngumu ya kiuchumi ambayo imesababishwa na msukosuko wa kiuchumi duniani. Kwa hiyo  ushuru kwa bidhaa za msingi kwa familia kama vile sabuni, sukari, mafuta ya kupika na ya magari utabaki vilevile. Serikali za Tanzania, Kenya na Uganda zawasilisha bajeti kuu

Baadhi ya wananchi wamelezea kuridhishwa na bajeti hiyo lakini wakataka serikali izidi kuweka mikakati ya kupunguza bei za mahitaji ya msingi ambazo kwa sasa zimepelekea hali ya maisha kuwa ngumu ikilinganishwa na mapato yao.

Uganda Kampala | Coronavirus | Straßenverkäufer
Mfanyabiashara wa Uganda akiwa anauza nyanya sokoniPicha: Getty Images/AFP/B. Katumba

Kwa mujibu wa maoni ya raia wengine, matarajio yao ilikuwa bajeti ambayo inaleta matumaini ya uchumi kuboreka na kuwakinga dhidi ya vyanzo vya kudorora kwa uchumi duniani, waweze kuingiza kipato zaidi kuanzia sekta za biashara hadi watumishi wa umma kuongezewa mishahara. Katika kipindi cha hivi karibuni, makundi kadhaa ya wafanyakazi wameshiriki migomo wakidai nyongeza ya mishahara. Bajeti ambayo imesomwa leo imetaja kuwaongezea fungu wafanyakazi wa afya na hilo limewafurahisha baadhi yao.

Kwa upande wake, rais Yoweri Museveni  amekariri azma yake ya kuhakikisha kwamba serikali inafadhili miradi ya maendeleo hasa barabara badala ya kuwategemea wafadhili wa kigeni.

Museveni ameongezea kuwa Uganda inazingatia sana usalama wa wananchi na hata kama kuna hali ya msukosuko kwenye mipaka yake na jamhuri ya kidemokrasia ya congo kule Kusini magharibi eneo la Bunagana, wananchi wasiwe na wasiwasi. Hii leo Uganda ilifungia magari ya mizigo kuvuka mpaka kwenda Congo kupitia eneo hilo ambalo hapo jana lilitekwa na wapiganaji wa M23.