1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAfrika Kusini

Ramaphosa atangaza baraza jipya la mawaziri

1 Julai 2024

Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa ametangaza baraza jipya la mawaziri huku vyama vya upinzani vya zamani vikijizolea nyadhifa 12 kati ya 32.

https://p.dw.com/p/4hjBZ
Cyril Ramaphosa akihudhuria hafla ya kula kiapo kwa muhula wake wa pili kama Rais wa Afrika Kusini.
Cyril Ramaphosa akihudhuria hafla ya kula kiapo kwa muhula wake wa pili kama Rais wa Afrika Kusini.Picha: Kim Ludbrook/Pool/EPA

Chama tawala cha African National Congress, ANC, ambacho kimetawala nchi hiyo kwa miaka 30, kimebaki na nafasi 20 kati ya hizo, zikijumuisha wizara muhimu za mambo ya nje, fedha, ulinzi, sheria na polisi.

Chama kikubwa katika muungano huo, Democratic Alliance (DA), kitashikilia nyadhifa sita zikiwemo mambo ya ndani, mazingira pamoja na ujenzi na usimamizi wa majengo ya serikali. Kiongozi wa DA John Steenhuisen, 48 mwenye umri aliteuliwa kuwa Waziri wa Kilimo.

Soma pia: Rais Ramaphosa hatimaye ateua baraza jipya la mawaziri

Ramaphosa amesema "Ni muhimu kuwaweka katika nafasi za uwajibikaji watu wanaojituma, wenye uwezo na wachapakazi, na ambao pia wana uadilifu. Tumelazimika kuhakikisha kuwa vyama vyote vina uwezo wa kushiriki ipasavyo katika utendaji wa kitaifa pia. Kama katika nyadhifa mbalimbali za bunge, na kwamba wanapaswa kuwakilisha utofauti wa watu wa Afrika Kusini ipasavyo."

Chama cha Inkatha Freedom Party (IFP), chama kinachopinga uhamiaji cha Patriotic Alliance na chama cha mrengo wa kulia cha Freedom-Front Plus na vyama vingine vidogo vilipata nafasi sita za baraza la mawaziri.