1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais wa Ujerumani alivyosubirishwa uwanja wa ndege Qatar

1 Desemba 2023

Kusimama akiwa amekunja mikono yake kwenye milango ya ndege siyo namna Rais wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier alivyofikiri angetumia karibu dakika 30 za ziara yake ya saa tatu mjini Doha.

https://p.dw.com/p/4Ze9r
Qatar Doha Frank-Walter Steinmeier akisubiri kwenye ndege
Rais wa Ujerumani Steinmeier (kushoto) alikwenda Doha kuzungumza na maafisa wa Qatar kuhusu kuiachiwa kwa mateka wanaoshikiliwa na Hamas.Picha: Rosalia Romaniec/DW

Jua liliwaka. Zulia jekundu lilikuwa limetandazwa. Gwaride la heshima la kijeshi lilikuwa tayari. Hata balozi wa Ujerumani nchini Qatar, Lothar Freischlader, alikuwapo. Tatizo pekee, hakuna afisa wa Qatar aliyekuwa amekuja kumkaribisha rasmi Rais wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier mjini Doha.

Akiwasili mapema kabla ya muda uliopangwa, Steinmeier alisubiri kwenye jua kali kwenye mlango wa ndege ya jeshi la Ujerumani Bundeswehr chapa ya Airbus A350, kwa karibu nusu saa kabla ya Sultan al-Muraichai, waziri wa mambo ya nje wa Qatar kuwasili kumpokea mkuu huyo wa nchi wa Ujerumani.

Pamoja na kucheleweshwa kwa taratibu za kidiplomasia kufuatia kuwasili kwa al-Muraichai, Steinmeier aliondoka uwanja wa ndege kwa wakati kwa mkutano wake uliopangwa na amiri mkuu wa Qatar, Sheikh Tamim bin Hamad Al Thani.

Zaidi ya dakika 30 za mchanganyiko?

Vurugu hizo za kidiplomasia zilimwacha mwandishi wa habari wa DW Rosalia Romaniec, ambaye alikuwa akisafiri na Steinmeier, akijiuliza kama kulikuwa na makosa katika mipango hiyo au ikiwa maafisa katika taifa hilo la Kiarabu waliamua kuisusia Ujerumani baada ya Steinmeier kutumia muda mwingi wa safari yake ya siku tatu katika eneo hilo nchini Israel, ikifuatiwa na nyusiku mbili nchini Oman na saa tatu tu katika taifa hilo la Ghuba.

Bundespräsident Steinmeier in Katar
Rais Steinmeier akiasalimia na Emir wa Qatar Tamim bin Hamad Al Thani waakti wa ziara yake ya Mashariki ya Kati, Novemba 29, 2023.Picha: Bernd von Jutrczenka/dpa/picture alliance

Nchini Ujerumani, ushawishi wa Doha katika vita vya Israel na Hamas unaonekana kuwa na utata kwani Qatar ni nyumbani kwa tawi la kisiasa la Hamas. Hilo liliwafanya baadhi ya watu kujiuliza iwapo kashfa hiyo ya Jumatano ilikuwa jibu kwa kauli zilizotolewa hivi karibuni na Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Annalena Baerbock kabla ya ziara iliyopangwa kwa muda mrefu ya Al Thani mjini Berlin mwezi Oktoba.

Soma pia: Rais Steinemeier ashuhudia ubunifu wa vijana wa Tanzania

"Hatukubali kuunga mkono ugaidi," Baerbock aliambia shirika la utangazaji la ZDF wakati huo. "Ili kukomesha ugaidi huu," aliongeza, "nchi kama Qatar zina jukumu maalum."

Qatar ilielezwa kukasirishwa na matamshi hayo. Nchi hiyo pia inaaminika kutuma kiasi kisichopungua dola bilioni 1.5 Ukanda wa Gaza unaodhibitiwa na Hamas kufadhili, kwa sehemu, malipo ya mishahara ya wafanyikazi wa hospitali na  wa utawala. Qatar imesema uhamisho wa fedha unafanywa kwa idhini ya Israel.

Qatar: Mpatanishi muhimu

Qatar tayari "imetumia ushawishi wake katika kanda hiyo na pia kwa Hamas" kupatanisha mapatano kati ya pande zinazozozana, Steinmeier aliongeza, akimaanisha mapatano yaliyofikiwa ambayo hadi sasa yamesitishwa vita kwa siku kadhaa kati ya Hamas na Israel, pamoja na kubadilishana mateka walioshikiliwa huko Gaza tangu mashambulizi ya Oktoba 7 kwa wafungwa wa Kipalestina waliokuwa wakishikiliwa katika jela za Israel.

Bundespräsident Steinmeier in Katar
Rais Steinmeier akizungumza na waandishi baada ya kukamilika kwa ziara yake ya Mashariki ya Kati, Novemba 29, 2023.Picha: Bernd von Jutrczenka/dpa/picture alliance

Kwa jumla, wafungwa zaidi ya 200 wa Kipalestina wameachiliwa kutoka jela za Israel, huku Hamas ikiwaachilia zaidi ya mateka 104, wakiwemo Waisrael 72.

Vita vya hivi sasa vya Gaza vilianza baada ya takriban watu 240 kuchukuliwa mateka na 1,200 kuuawa na Hamas katika mashambulizi yake ya Oktoba 7 kusini mwa Israel. Ujerumani, Marekani, Israel na mataifa mengine kadhaa pamoja na Umoja wa Ulaya wanaiorodhesha Hamas kama shirika la kigaidi.

SomaJe, ukomo wa deni la Ujerumani ni nini hasa?

Israel ilijibu kwa mashambulizi makubwa ya anga na mzingiro wa Ukanda wa Gaza kabla ya vikosi vyake vya jeshi kuanza mashambulizi ya ardhini mwishoni mwa Oktoba. Operesheni za kijeshi za Israel zimeua zaidi ya watu 14,800 katika Ukanda wa Gaza, kulingana na Wizara ya Afya inayoongozwa na Hamas.

Qatar ilikuwa kituo cha mwisho cha ziara ya Steinmeier katika eneo hilo, ambapo alianzia Israel, alikokutana na Rais Isaac Herzog na jamaa za waliochukuliwa mateka katika Ukanda wa Gaza, na kusimama nchini Oman siku ya Jumanne.

Si Qatar, Steinmeier wala maafisa wa Ujerumani waliozungumzia ucheleweshaji wa kidiplomasia usiokuwa wa kawaida katika uwanja wa ndege.