1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mazungumzo ya Paris kuleta matumaini kwa mateka wa Gaza

30 Januari 2024

Waziri wa Mambo ya Kigeni wa Marekani Antony Blinken ameelezea matumaini ya kupatikana muafaka wa kusitishwa mapigano kati ya Israel na Hamas huko Gaza kwa kubadilishana na kuwachiliwa huru mateka.

https://p.dw.com/p/4boqw
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken
Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony BlinkenPicha: Evelyn Hockstein/REUTERS

Hii ni baada ya kufanyika mazungumzo mjini Paris yakimhusisha mpatanishi Qatar. Blinken amewaambia waandishi habari baada ya kukutana mjini Washington na waziri mkuu wa Qatar kuwa kazi muhimu sana na yenye tija imefanyika na kuna matumaini ya kweli ya kusonga mbele.

Mkutano huo wa Jumapili mjini Paris uliwakutanisha mkuu wa shirika la Ujasusi la Marekani - CIA William Burns na maafisa kutoka Israel, Misri na Qatar, ambayo ni mshirika wa Marekani.

Soma pia:Watu 215 wauawa Gaza katika kipindi cha saa 24 zilizopita

Waziri Mkuu wa Qatar Sheikh Mohammed bin Abdulrahman Al Thani, aliyehudhuria mazungumzo hayo, amesema hatua nzuri zimepigwa na pande zote zinatumai kuwasilisha pendekezo hilo kwa Hamas na kuwafikisha katika mahali ambapo watashiriki kwa njia chanya na yenye tija katika mchakato huo.