1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
JamiiMamlaka ya Palestina

Watu 215 wauawa Gaza katika kipindi cha saa 24 zilizopita

29 Januari 2024

Wizara ya afya katika Ukanda wa Gaza imesema kwamba takriban watu 26,637 wameuwawa katika eneo hilo la Palestina katika vita kati ya kundi la wanamgambo la Hamas na Israel.

https://p.dw.com/p/4bnxA
Wakaazi katika ukanda wa Gaza
Wakaazi katika ukanda wa GazaPicha: Khaled Omar/Xinhua/picture alliance

Taarifa ya wizara hiyo imesema idadi hiyo inajumuisha vifo vya watu 215 vilivyotokea ndani ya kipindi cha saa 24 zilizopita, huku watu 65,387 wakiwa wamejeruhiwa tangu vilipozuka vita hivyo Oktoba 7.

Wakati huo huo, waziri wa usalama wa Israel kutoka kambi ya wenye misimamo mikali, Itamar Ben Gvir amewatolea mwito walowezi wa Kiyahudi kurejea Gaza.

Matamshi ya waziri huyo yaliyotolewa jana mbele ya mkusanyiko mkubwa, yameibuwa kauli za hasira kutoka kwa Wapalestina wanaosema yanaongeza makali ya mwito unaolenga kuwalazimisha Wapalestina waihame ardhi yao.

Kauli ya waziri huyo wa usalama wa Israel inapishana na msimamo wa serikali uliotolewa na waziri mkuu Benjamin Netanyahu uliosisitiza kwamba Israel haina dhamira ya kuikalia Gaza.

DW Kiswahili | Saumu Mwasimba
Saumu Mwasimba Mhariri na mtangazaji wa Idhaa ya Kiswahili ya DW