1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Jimbo la Kivu Kusini lahitaji dola Mil. 56 kujijenga upya

Admin.WagnerD31 Mei 2024

Imefahamika kuwa jimbo la Kivu Kusini mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo linahitaji angalau dola milioni 56 kuweza kukabiliana na matatizo ya kiusalama na miundombinu.

https://p.dw.com/p/4gVc4
DR Kongo | Ujumbe wa kulinda amani, MONUSCO
MMoja ya wanajeshi wa kulinda amani wa Umoja wa Mataifa akiwa kwenye harakati zake kaskazini mwa Goma, nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya KongoPicha: Moses Sawasawa/AP Photo/picture alliance

Tathmini hii imetangazwa kufuatia ziara ya Ujumbe wa Wafadhili wa Kongo unaoongozwa na Mratibu Mkaazi wa Umoja wa Mataifa nchini Kongo, Bruno Lemarqui katika jimbo hilo ili kutathmini hali ya mambo na kuhakikisha maendeleo na utulivu pale MONUSCO itakapoondoka. 

Ujumbe huu unaundwa na washirika yapata ishirini wa kiufundi na kifedha wa Kongo wakiwemo wakuu wa ushirikiano kati ya Kongo na nchi mbalimbali, wawakilishi wa Umoja wa Ulaya, Benki ya Dunia, MONUSCO na mashirika na taasisi za Umoja wa Mataifa, ambayo kwa pamoja wanaunda kile kinachoitwa "Kundi la Uratibu wa Washirika".

Mbele ya wanahabari mjini Bukavu, Mratibu mkazi wa Umoja wa Mataifa nchini Kongo Bruno Lemarquis alisema "Ujumbe huu wa pamoja uliundwa katika muktadha wa MONUSCO kuondoka Kivu Kusini ifikapo Juni 30, na bila shaka katika muktadha mpana wa changamoto zinazolikabili jimbo hili; za kiusalama katika baadhi ya maeneo kwa mfano wilaya ya Kalehe inayoathirika na mgogoro wa M23." 

DRC | Daktari Denis Mukwege akizungumza mjini Bukavu
Daktari Denis Mukwege anayewasaidia wanawake waliodhulumiwa kingono nchini Kongo ameelezea wasiwasi baada ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa kuondoka nchini humoPicha: Ernest Muhero/DW

Soma pia: Usalama mashariki mwa Kongo waazidi kuzorota huku kundi la waasi yakijiimarisha

Mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, mwaka 2018, Daktari Denis Mukwege yeye alisema kuondoka kwa MONUSCO kutachochea uporaji wa maliasili ya Kongo.

Ujumbe huu uliwatembelea pia wanawake waathirika wa dhuluma za ngono na ubakaji wanaotibiwa kwenye hospitali ya Panzi ya Daktari Mukwege.

Ujumbe huo umekumbusha kwamba mara baada ya MONUSCO kuondoka, serikali ya Kongo itawajibika kuhusu usalama wa raia wake na shughuli nyingine muhimu zilizokuwa zikifanywa na MONUSCO hapo awali.

Soma pia: Kuna jumla ya makundi 266 yanayomiliki silaha mashariki ya Kongo