1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroMamlaka ya Palestina

Miito yaongezeka ya kuwepo taifa huru la Palestina

22 Januari 2024

Viongozi mbalimbali ulimwenguni wametoa miito ya usitishwaji mapigano huko Gaza na kuwepo kwa suluhisho la mataifa mawili ya Israel na Palestina na kusema kuwa hiyo ndio njia pekee ya kuwepo amani ya kudumu eneo hilo.

https://p.dw.com/p/4bXD4
Kongamano la Fatah- Mahmoud Abbas
Rais wa Mamlaka ya Palestina Mahmoud Abbas akiwasalimia wafuasi wa chama cha Fatah katika kongamano la vuguvugu hilo katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu:04.08.2009Picha: AP

Israel ambayo imeapa kulitokomeza kundi hilo, imetupilia mbali miito ya uwepo wa taifa huru la Palestina na kusema wataendelea kuwa na udhibiti wa usalama huko Gaza hata baada ya vita hivyo kumalizika.

Mshirika wake mkuu, Marekani na nchi nyingine kadhaa, wamependekeza kwamba suluhisho la mataifa mawili ndio njia pekee ya kuhakikisha usalama wa kudumu wa pande zote.

Kabla ya mkutano na wajumbe wa Israel na Palestina, Mkuu wa sera za kigeni wa Umoja wa Ulaya Josep Borrell amesisitiza juu ya suluhisho la mataifa mawili na kusema Israel haiwezi kudumisha amani kwa kwa mtuto wa bunduki. Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Annalena Baerbock amesema uwepo wa mataifa mawili ya Israel na Palestina ndio suluhu pekee katika mzozo huo wa Mashariki ya Kati.

Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Annalena Baerbock
Waziri wa mambo ya nje wa Ujerumani Annalena Baerbock alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari: 11.01.2024Picha: Michael Kappeler/dpa/picture alliance

" Israel wataweza kuishi kwa usalama ikiwa tu Wapalestina nao wataishi kwa usalama na kwa heshima. Na Wapalestina wanaweza kuishi kwa heshima, kwa usalama na kwa uhuru ikiwa Israel itaweza kuishi kwa usalama. Ndio maana suluhu la mataifa mawili ndilo suluhu pekee, na wale wote wanaokataa kutambua hilo hadi sasa hawajapendekeza njia mbadala.”

Soma pia: Hamas: Zaidi ya watu 25,000 wameuwawa wakati Israel ikiendeleza mashambulizi yake Gaza

Mawaziri 27 wa mambo ya nje wa Umoja wa Ulaya watakutana na waziri wa mambo ya nje wa Israel Israel Katz, kabla ya kuzungumza na mwanadiplomasia mkuu wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina Riyad al-Maliki. Mawaziri wa mambo ya nje wa Misri, Jordan na Saudi Arabia pia watafanya mazungumzo na mawaziri hao wa Ulaya.

Mashambulizi yaendelea huko Gaza

Vita Gaza- Mji wa Khan Younis
Moshi ukifuka kutoka mji wa Khan Younis kusini mwa Ukanda wa Gaza kufuatia shambulizi la Israel: 02.01.2024Picha: AFP/Getty Images

Mapambano makali kati ya jeshi la Israel na wanamgambo wa Hamas yameripotiwa usiku wa kuamkia leo katika mji wa kusini mwa Gaza wa Khan Younis. Ghasia zimeongezeka pia katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu na Israel.

Katika ripoti yake ya kwanza kwa umma, kundi la Hamas lilikiri baadhi ya makosa katika matukio ambayo yalianzisha vita hivyo lakini pia likatoa wito wa kukomeshwa kwa kile walichokiita "uchokozi wa Israel" huko Gaza. Hamas imedai shambulio la Oktoba 7 ilikuwa "hatua muhimu" dhidi ya uvamizi wa Israel katika maeneo ya Wapalestina.

Soma pia: Netanyahu anapinga wazo la kuipa mamlaka ya Palestina udhibiti katika ukanda wa Gaza

Familia za mateka takriban 132 ambao bado wanashikiliwa huko Gaza wamemtaka Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu kufikia makubaliano na kundi la Hamas ili mateka hao waweze kuachiliwa huru.

Netanyahu amesema Hamas wametoa masharti ya kuachiwa mateka hao ambayo hayakubaliki. Hamas inataka vita visitishwe, kuondolewa kwa vikosi vyote vya Israel huko Gaza, kuachiliwa kwa wafungwa wa Kipalestina na kuhakikishiwa itasalia madarakani.

(Vyanzo: Mashirika)