1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaIsrael

UNICEF "Gaza eneo hatari zaidi kwa watoto"

19 Desemba 2023

Shirika la Kimataifa la Kuwahudumia Watoto - UNICEF limesema Gaza ni eneo hatari zaidi kwa watoto kuishi na kuwalaumu wenye mamlaka kwa kupuuza madhila ya kibinaadamu yanayowakumba mamilioni ya watoto kwenye eneo hilo.

https://p.dw.com/p/4aLlh
Watoto wa Ukanda wa Gaza katika kambi ya wakimbizi ya Jebaliya
Watoto wa Kipalestina wakiuza pipi mbele ya vifusi vya jengo lililoharibiwa katika kambi ya wakimbizi ya Jebaliya, Ukanda wa Gaza, Novemba 28, 2023, katika siku ya tano ya usitishwaji vita kati ya Hamas na Israel.Picha: Mohammed Hajjar/AP Photo/picture allinance

UNICEF linasema haya wakati Shirika la Afya, WHO likisema hali mbaya kabisa kwenye eneo hilo haijashuhudiwa bado mahala popote ulimwenguni. 

Wakiwa mjini Geneva, wasemaji kutoka UNICEF, James Elder na Margareth Harrison, wamezungumzia hali mbaya katika Ukanda wa Gaza tangu israel ilipoanzisha mashambulizi ya kisasi dhidi ya kundi la Hamas lililoishambulia kwanza mnamo Oktoba 7.

Elder amesema Gaza ni mahala pa hatari zaidi ulimwenguni kwa sasa na hapafai kwa watoto kuishi. Elder aliyerejea Geneva akitokea Gaza, amesema hayo huku akieleza kuchukizwa na viongozi ambao amesema hawajali namna ambavyo watoto wanaathirika kutokana na mashambulizi hayo.

Elder alisema "Nina hasira. Nina hasira kwamba wale walio na mamlaka wanapuuzia wakati jinamizi la kibinadamu linalowatafuna watoto milioni moja. Nina hasira kwamba watoto wanaopona majeraha baada ya kukatwa viungo wanauawa wakiwa hospitalini."

Soma pia: Papa Francis aomboleza kifo cha "raia wasio na ulinzi" ukanda wa Gaza

Mji wa Gaza | Wafanyakazi wa tiba katika Hospitali ya Al-Ahli Baptist huko Gaza
Wahudumu wa afya wakiwahudumia Wapalestina waliojeruhiwa wakiwemo watoto, nje ya Hospitali ya Al-Ahli Baptist huku baadhi ya maeneo ya hospitali hiyo yakiharibiwa baada ya mashambulizi ya anga ya Israel la Novemba 15, 2023.Picha: Montaser Alswaf/Anadolu/picture alliance

Alikuwa akiwazungumzia watoto waliokatwa viungo na baadae kuuawa wakiwa kwenye hospitali ambazo pia zilishambuliwa. Amesema hospitali ya Nasser ambayo pekee ndio iliyokuwa ikiendelea kutoa huduma, katika mji mkuu wa kusini mwa Gaza wa Khan Younis imeshambuliwa mara mbili katika kipindi cha masaa 48 yaliyopita. Alisema "Nina hasira kwamba kuna watoto zaidi ambao sasa wamejificha mahali fulani ambao bila shaka watapigwa na kukatwa viungo siku zijazo."

Hospitali ya Nasser ilikuwa ikihifadhi watoto na wanawake

Hospitali hiyo kulingana naye, sio tu ilikuwa inahifadhi idadi kubwa ya watoto ambao tayari walikuwa wamejeruhiwa vibaya baada ya kushambuliwa majumbani kwao, bali pia mamia ya wanawake na watoto waliokuwa wakitafuta mahala salama pa kujihifadhi.

Lakini si yeye tu aliyezungumzia madhila yanayowakumba watu wa Gaza, bali pia msemaji wa shirika la Afya ulimwenguni, Margareth Harrison alisema hata wafanyakazi wenzake wanakiri kwamba hawajawahi kushuhudia kile kinachoendelea sasa kwenye eneo hilo la Palestina.WHO

Harrison alisema "Mfanyakazi mwenzangu alituambia watu walikuwa wamelala sakafuni wakiwa na maumivu makali, wakiwa na uchungu...lakini hawakuomba dawa ya kutuliza maumivu. Walikuwa wakiomba maji."

Mtumishi wa afya huko Gaza
Sehemu ya Hospitali ya Nasser iliyoko Khan Yunis, Gaza mnamo Desemba 11, 2023. Madaktari na wauguzi wanaofanya kazi katika hospitali hiyo wanafanya kazi kwa muda wa ziada kuwatibu Wapalestina waliojeruhiwa katika mashambulizi ya Israel.Picha: Abed Zagout/picture alliance/Anadolu

Wizara ya afya ya Gaza yasema shambulizi la Israel liliwaua watu 20

Wizara ya Afya ya Gaza imesema kwamba shambulizi la Israel liliwaua watu 20 huko Rafah. Na Shirika la habari la AP liliripoti likiwanukuu waandishi walioko huko kwamba shambulizi katika makazi yaliyowahifadhi raia lilisababisha vifo vya karibu watu 25.

Na taarifa kutoka huko Israel zimesema mapema leo kwamba kulisikika ving'ora vya tahadhari katika mji wa Tel Aviv baada ya wanamgambo wa Hamas kusema walirusha mkururo wa maroketi kuelekea kwenye mji huo wa pwani.

Ving'ora pia vililia katika miji ya Jaffa, Bat Yam, Rishon Lezion, Kfar Chabad na Beit Dagan. Jeshi la Israel, IDF, liliandika kwenye ukurasa wake wa X kwamba hata baada ya siku 74 za vita dhidi ya Hamas, ving'ora vimesikika katikati mwa Israel na mamilioni ya Waisrael walikimbilia mafichoni.

Hata hivyo hakukua na ripoti za uharibifu yoyote.

Kundi la Hamas, limeorodheshwa na Israel, Marekani, Ujerumani, Umoja wa Ulaya na mataifa mengine kuwa ni la kigaidi.