1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

Waziri mkuu wa zamani Pakistan ahukumiwa miaka 10 jela

30 Januari 2024

Mahakama maalum Pakistan, yamkuta na hatia Waziri Mkuu wa zamani Imran Khan ya kuvujisha siri nyeti za serikali kwa umma na kumuhukumu kifungo cha miaka 10 jela. Chama chake kimesema kitakata rufaa.

https://p.dw.com/p/4bp5s
Pakistan | Waziri Mkuu wa zamani Imran Khan
Waziri mkuu wa zamani wa Pakistan Imran KhanPicha: Mohsin Raza/REUTERS

Hukumu hiyo imetolewa leo Jumanne na mahakama maalum mjini Islamabad ikiwa zimebaki siku 10 nchi hiyo iingie kwenye uchaguzi mkuu.

Hukumu ya kifungo cha miaka 10 dhidi ya waziri mkuu wa zamani Imran Khan imewaghadhabisha wanasiasa kwenye chama chake cha  Pakistan Tehreek e-Insaf,kinachosema ni hukumu kali kabisa kuwahi kutolewa hadi sasa dhidi ya mwanasiasa huyo wakati nchi ikijiandaa kuingia kwenye uchaguzi mkuu.

Mahakama maalum iliyokuwa ikisikiliza kesi hiyo imemkuta Imran Khan na hatia ya kuvujisha kwa umma siri za serikali zilizokuwa kwenye ujumbe uliotumwa kwa serikali ya Islamabad  na balozi wa Pakistan mjini Washington.

Kesi hiyo pia imemuhusisha waziri wa zamani wa mambo ya nje Shah Mehmood Qureshi aliyehukumiwa kifungo cha miaka 10.

Wakili wa Imran Khan, Naeem Panjutha  amesema hawakubaliani na uamuzi huo wa mahakama ambao kwa mtazamo wao sio halali na kwamba chama cha PTI, yaani Pakistan Tarek-e-Insaf cha mwanasiasa huyo kitachukua hatua kuupinga uamuzi wa Mahakama.

Soma Pia:Imran Khan anazuiwa gerezani tangu mwezi Agosti baada ya kukumbwa na hatia ya ufisadi

Msaidizi wa Khan, Zulfikar Bukhari ameliambia shirika la habari la Reuters kwamba timu ya wanasheria ya mwanasiasa huyo haikupewa nafasi yoyote kumuwakilisha waziri mkuu huyo wa zamani au kuwahoji mashahidi waliotumiwa na juu ya hilo mchakato mzima wa kesi hiyo ulioendeshwa gerezani alikozuiliwa bwana Khan.

Kwa hivyo anasema hukumu hiyo inaonesha wazi ni juhudi za kudhoofisha uungwaji mkono wa Khan.

Hukumu inatolewa siku chache kabla ya uchaguzi

Uchaguzi mkuu nchini Pakistan unatarajiwa kufanyika katika kipindi cha siku 10 zijazo na msaidizi huyo wa Imran Khan anasema hivi sasa Wapakistan watahakikisha wanajitokeza kwa wingi kabisa kupiga kura.

Wafuasi wa chama cha PTI
Wafuasi wa chama cha imran Khan cha Tehrik-e-InsafPicha: Saood Rehman/EPA/picture alliance

Chama cha PTI kilichoshinda uchaguzi wa mwaka 2018 kilipata pigo kubwa mwanzoni mwa mwezi Januari baada ya  mahakama  kuidhinisha uamuzi wa tume ya uchaguzi wa kukifutia chama hicho nembo yake ya tangu zamani ya kushiriki kwenye uchaguzi ambayo ni ''alama ya gongo la mchezo wa Kriketi'' .Soma Pia: Kwanini Wapakistan hawajali kuhusu uchaguzi ujao

Ili chama kishiriki kwenye uchaguzini,ni lazima nchini Pakistan kiwe na nembo iliyoidhinishwa na tume  ya kukitambulisha kwenye debe la uchaguzi.

Kutokana na pigo hilo hivi sasa wagombea wa chama hicho wanasimama kama wagombea binafsi huku wengi wao wakihangaika kujifichakufuatia kile ambacho chama imekiita ni kuandamwa na vyombo vya usalama vinavyoungwa mkono na jeshi,Japo jeshi linayakanusha madai haya.

Imran Khan anayekabiliwa na matatizo na nyota wa zamani wa mchezo wa Kriketi aliwahi huko nyuma kuhukumiwa kwenda jela miaka 3 katika kesi inayohusu ufisadi ambayo ilichangia kuondolewa kwake katika orodha ya wagombea wa uchaguzi mkuu wiki ijayo.

Lakini timu yake ya kisheria ilikuwa na matarajio ya kumtoa jela ambako anashikiliwa tangu mwezi Agosti mwaka jana.

Hata hivyo hukumu hii iliyotolewa leo ya kifungo cha miaka 10 inamaanisha kwamba hakuna uwezekano wa kuachiliwahata ikiwa mashataka yanayomkabili yatapelekwa  katika mahakama ya juu zaidi

Imran Khan ana kiu ya kukomesha machafuko Pakistan

 

DW Kiswahili | Saumu Mwasimba
Saumu Mwasimba Mhariri na mtangazaji wa Idhaa ya Kiswahili ya DW