1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Biden ziarani Ireland Kaskazini

Angela Mdungu
12 Aprili 2023

Rais wa Marekani Joe Biden yuko ziarani Ireland ya Kaskazini akihudhuria kumbukumbu ya miaka 25 ya makubaliano ya Ijumaa kuu yaliyorejesha amani katika eneo hilo ambalo ni sehemu ya Uingereza

https://p.dw.com/p/4PweY
UK | US-Präsident Biden besucht Nordirland
Picha: Patrick Semansky/AP/picture alliance

 Makubaliano hayo yalifanikiwa baada ya Marekani kusaidia kufanyika kwa mazungumzo ya usuluhishi ya kumaliza machafuko yaliyouwa maelfu ya watu.

Katika ziara yake ya kwanza Ireland ya Kaskazini tangu alipoingia madarakani Biden anatarajiwa pia kukutana na waziri mkuu  wa Uingereza Rishi Sunak.

Biden atapata pia nafasi ya kutoa salamu za pongezi na kuwahimiza viongozi wa nchi hiyo kuzifanyia kazi sera za uchumi na biashara zenye manufaa kwa wote.

Anatarajiwa kusalimiana na viongozi wa vyama vya siasa vinavyokinzana vya Ireland Kaskazini, kabla ya kutoa hotuba katika kampasi mpya ya chuo cha Ulster kwenye mji mkuu Belafast.

Mitazamo tofauti ziara ya Biden

Hata hivyo baadhi ya wanachama wa ngazi ya juu wa chama kinachounga mkono demokrasia cha DUP kilicho kwenye shinikizo la kuanzisha tena mgawanyo wa madaraka wa ndani, hawakuwa na maoni ya chanya kuhusu ujio wa Biden.

Mmoja wa wanachama wa chama hicho ambaye pia ni mbunge katika bunge la Wesminster Sammy Wilson amemtaja Biden kuwa mtu asiyeiunga mkono Uingereza.

Ireland Kaskazini haina serikali thabiti. Bunge lake lijulikanalo kama Stormont liliahirishwa tangu chama cha DUP ambacho nusu yake ilikuwa ikiunda serikali kilipojitoa kutokana na mzozo uliojitokeza baada ya Uingereza kujitoa katika nchi za umoja wa Ulaya.

Pichani ni waziri mkuu wa Uingereza Rishi Sunak na Rais wa Marekani Joe Biden
Waziri mkuu wa Uingereza Rishi Sunak na Rais wa Marekani Joe Biden Picha: Valeria Ferraro/SOPA/ZUMA Press/picture alliance

Kujitoa kwa Uingereza kwenye umoja huo kuliiweka Ireland ya Kaskazini katika nafasi ngumu kati ya nchi nyingine za Uingereza na Ireland ambayo ni mwanachama wa Umoja wa Ulaya. Hali hiyo iliongeza doa katika makubaliano ya amani yaliyofanyika miaka 25 iliyopita.

 

Chanzo: APE/AFP