1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Zelenskiy aamuru watu waondoke Donetsk

31 Julai 2022

Rais wa Ukraine amewaamuru wakaazi kuondoka mara moja katika eneo la mashariki la Donetsk. Wakati huo huo, Kyiv imesema jeshi la Ukraine liliua askari wengi wa Urusi huko Kherson.

https://p.dw.com/p/4Euvc
Ukraine Krieg Zerstörun in Kramatorsk
Picha: Anatolii StepanovAFP/Getty Images

Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskiy Jumamosi aliamuru kuhamishwa kwa watu kutoka eneo la mashariki la Donetsk ambalo limeshuhudia mapigano makali kati ya vikosi vya Urusi na Ukraine.

"Tayari kuna uamuzi wa serikali kuhusu uhamishaji wa lazima kutoka mkoa wa Donetsk," Zelenskiy alisema katika hotuba yake ya kila siku ya video. "Tafadhali, fuateni uhamishaji. Katika awamu hii ya vita, ugaidi ni silaha kuu ya Urusi."

Soma zaidi: Zelensky ashuhudia upakiaji wa nafaka Odesa

Alisema mamia kwa maelfu ya watu bado wanaishi katika maeneo ya Donbas ambako mapigano yalikuwa makali.

"Ikiwa utapata fursa, tafadhali zungumza na wale ambao bado wamesalia katika maeneo ya mapigano huko Donbas. Tafadhali washawishi kwamba ni muhimu kuondoka, haswa ikiwa ni familia zenye watoto. Ukipata fursa ya kusaidia watu waliohamishwa, fanya hivyo. hilo,” alisema.

ARCHIV | Ukraine Kiew | Präsident Wolodomyr Selenskyi
Rais wa Ukraine Volodymyr Zelenskiy.Picha: Valentyn Ogirenko/REUTERS

Zelenskyy aliahidi msaada wa vifaa na pesa taslimu kusaidia wakaazi wanaohamishwa.

Katika tukio tofauti, vyombo vya habari vya Ukraine vilimnukuu Naibu Waziri Mkuu Iryna Vereshchuk akisema uhamishaji unahitajika kufanyika kabla ya msimu wa baridi kuanza kwa sababu usambazaji wa gesi asilia katika eneo hilo uliharibiwa.

Mapema siku ya Jumamosi, jeshi la Ukraine lilisema zaidi ya wanajeshi 100 wa Urusi wameuawa na vifaru saba kuharibiwa katika mapigano kusini siku ya Ijumaa, ikiwa ni pamoja na eneo la Kherson ambalo ndiyo shabaha ya mashambulizi ya kujibu ya Kyiv katika sehemu hiyo ya nchi na kiungo muhimu katika njia za usambazaji za Moscow.

Soma pia: Utafiti wa Yale: Vikwazo vyaathiri uchumi wa Urusi

Usafiri wa reli hadi Kherson kuvuka Mto Dnipro ulikuwa umekatwa, ilisema kamandi ya kusini ya jeshi, na kuweka uwezekano zaidi wa kuvitenga vikosi vya Urusi magharibi mwa mto na ugavi rasi inayokaliwa ya Crimea na mashariki.

Kusini mwa mji wa Bakhmut, ambao Urusi imeutaja kama shabaha kuu huko Donetsk, jeshi la Ukraine lilisema kuwa vikosi vya Urusi "vimefanikiwa kwa kiasi" kudhibiti eneo la makazi la Semyhirya kwa kulivamia kutoka pande tatu.

"Amejiimarisha nje kidogo ya makazi," ripoti ya jioni ya jeshi ilisema, ikimaanisha vikosi vya Urusi.

Ukraine-Konflikt, von Artillerie beschädigte Brücke in Cherson
Daraja la Kherson lililoharibiwa na makombora ya Ukraine.Picha: Sergei Bobylev/ITAR-TASS/IMAGO

UK: Urusi yapambana kudumisha kasi ya uvamizi

Maafisa wa ulinzi na ujasusi wa Uingereza, ambayo imekuwa moja wa washirika wakubwa wa Ukraine tangu Moscow ilipovamia jirani yake Februari 24, walivionyesha vikosi vya Urusi kama vinavohangaika kudumisha kasi.

Ukraine imetumia mifumo ya makombora ya masafa marefu inayotolewa na nchi za Magharibi

kuharibu vibaya madaraja matatu katika Mto Dnipro katika wiki za hivi karibuni, na kuukatia mawasiliano mji wa Kherson na - katika tathmini ya maafisa wa ulinzi wa Uingereza - kukiacha cha 49 cha jeshi la Urusi katika hatari kubwa kwenye ukingo wa magharibi wa mto huo.

Soma pia: Macron na Bin Salman kupunguza athari za vita Ukraine

Gavana wa mkoa wa Kherson anayeegemea Ukrainian, Dmytro Butriy, alisema mapigano yanaendelea katika maeneo mengi ya eneo hilo, na kwamba wilaya ya Berislav, kaskazini magharibi mwa kiwanda cha kuzalisha umeme cha Kakhovka, iliathirika sana.

"Katika baadhi ya vijiji, hakuna hata nyumba moja iliyoachwa, miundombinu yote imeharibiwa, watu wanaishi kwenye mahandaki," aliandika kwenye Telegram.

Ukraine I  Olenivka Gefängnis
Gereza la wafungwa wa kivita wa Ukraine lililoshambuliwa na kuuwa wafungwa wasiopungua 50 karibu na mji wa Olenivka.Picha: RIA Novosti/SNA/IMAGO

Kaskazini mwa Lysychansk, ambayo vikosi vya Moscow viliiteka mapema Julai baada ya mapigano ya wiki kadhaa, wapiganaji wa Ukraine waliharibu boksi la makutano ya reli karibu na mji unaodhibitiwa na Urusi wa Svatove Ijumaa usiku, na kuifanya iwe ngumu kwa Moscow kusafirisha risasi hadi uwanja wa mapigano kwa treni, gavana wa eneo la Luhansk Serhiy Gaidai alisema kwenye chapisho la mtandaoni.

Maafisa wa utawala ulioteuliwa na Urusi kuendesha mkoa wa Kherson, mapema wiki hii walipinga tathmini za Magharibi na Ukraine kuhusu hali hiyo.

Siku ya Ijumaa wizara ya Uingereza ilielezea serikali ya Urusi kuwa "inazidi kukata tamaa", ikiwa imepoteza makumi ya maelfu ya wanajeshi katika vita. Mkuu wa shirika la kijasusi la Uingereza MI6 Richard Moore aliongeza kwenye Twitter kwamba Urusi "inaishiwa na ari."

Vifo vya gerezani

Ukraine na Urusi zimetuhumiana kuhusu shambulizi la kombora au mlipuko mapema siku ya Ijumaa ambao ulionekana kuua makumi ya wafungwa wa vita wa Ukraine katika mji wa mapambano wa Olenivka, unaoshikiliwa na waasi wanaoungwa mkono na Moscow mashariki mwa Donetsk.

Soma pia: Ukraine yaanza tena shughulli za ugavi wa nafaka katika bandari

Wizara ya ulinzi ya Urusi siku ya Jumamosi ilichapisha orodha ya wafungwa 50 wa kivita wa Ukraine waliouawa na 73 waliojeruhiwa katika kile ilichosema ni shambulio la kijeshi la Ukraine kwa kutumia mfumo wa roketi wa kisasa uliotengenezwa na Marekani (HIMARS).

Msemaji wa wizara hiyo Luteni Jenerali Igor Konashenkov alisema "wajibu wote wa kisiasa, jinai na maadili unabaki kwa Zelenskiy, serikali yake ya uhalifu na Washington inayowaunga mkono".

Vikosi vya jeshi la Ukraine vilikanusha kuhusika, vikisema kwamba mizinga ya Urusi ililenga jela hiyo ili kuficha unyanyasaji wa wale wanaoshikiliwa humo. Waziri wa Mambo ya Nje Dmytro Kuleba alisema siku ya Ijumaa Urusi ilifanya uhalifu wa kivita na kutoa wito wa kulaaniwa kimataifa.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Antony Blinken alituma salaam za pole katika simu ya Ijumaa na Kuleba na kusema Washington imejitolea "kuiwajibisha Urusi kwa ukatili," wizara ya mambo ya nje ya Marekani ilisema.

Soma pia:Urusi yasema mashambulizi bandari ya Odessa yalilenga silaha za Marakeni 

Urusi imesema imewaalika wataalamu kutoka Umoja wa Mataifa na Shirika la Msalaba Mwekundu kuchunguza vifo hivyo.

Wizara ya Ulinzi ya Urusi ilisema katika taarifa Jumapili kwamba inataka ufanyike uchunguzi huru juu ya kile ilichokiita shambulio dhidi ya gereza mapema wiki hii.

Ukraine imeishutumu Urusi kwa ukatili dhidi ya raia na kubaini zaidi ya uhalifu wa kivita 10,000 unaowezekana. Urusi inakanusha kuwalenga raia na uhalifu wa kivita.

Chanzo: rtre