1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroIsrael

Zaidi ya watu milioni moja wakimbia Rafah

Saleh Mwanamilongo
3 Juni 2024

Shirika la Umoja wa mataifa la kuhudumia wakimbizi wa Kipalestina UNRWA limesema zaidi ya watu milioni moja wamelazimika kuuhama mji wa Rafah huko Ukanda wa Gaza kufuatia mashambulizi ya Israel.

https://p.dw.com/p/4gZia
Wakaazi wa Rafah wameukimbia mji huo kufuatia mashambulizi ya Israel
Wakaazi wa Rafah wameukimbia mji huo kufuatia mashambulizi ya IsraelPicha: Eyad Baba/AFP/Getty Images

Shrika la UNRWA lilisema Jumatatu (03.06.2024) kuwa maelfu ya familia sasa wanapata hifadhi katika maeneo na miundombinu zilizoharibiwa katika jiji la Khan Younis, ambapo shirika hilo linatoa huduma muhimu licha ya changamoto zinazoongezeka. Shirika hilo limesema linafanya kazi katika mazingira magumu.

Kulingana wizara ya afya ya Gaza watu wasiopungua 19 waliuwawa katika mashambulizi ya Israel usiku wa kuamkia leo, ikiwa ni pamoja na watu sita katika kambi ya wakimbizi ya Bureij.

Ni katika hali hiyo ndiyo waziri wa mambo ya nje wa Misri Sameh Shoukry amesema kwamba nchi yake imepinga uwepo wa Israel kwenye kivuko cha Rafah kwenye mpaka wa Misri na Ukanda wa Gaza.

Kwenye mkutano na waandishi habari na mwenzie wa Uhispania huko Madrid, Sameh Shoukri amesema ni vigumu kwa kivuko cha Rafah kuendelea kufanya kazi bila utawala wa Palestina. Aidha, waziri wa ulinzi wa Israel Yoav Gallant amesema Israel itaendelea na malengo yake huko Gaza.

"Sambamba na operesheni hii muhimu ya kijeshi, taasisi ya ulinzi na usalama kwa maelekezo yangu inaandaa mfumo mbadala wa uongozi wa Hamas, huku tukitenga maeneo, kuwaondoa viongozi wa Hamas katika maeneo haya na kuanzisha vikosi vingine vitakavyowezesha kuwepo kwa serikali mbadala ambayo itakuwa pia kitisho kwa Hamas.", alisema Gallant.

Marekani yaishinika Hamas kukubali mpango wa amani

Blinken azungumza na viongozi wa Israel kutaka usitishwaji mapigano
Blinken azungumza na viongozi wa Israel kutaka usitishwaji mapiganoPicha: Menahem Kahana/AP/picture alliance

Hata hivyo Marekani imendelea na juhudi zake za kuweko na usitishwaji mapigano huko Gaza. Waziri wa mambo ya nje wa Marekani Antony Blinken analishinikiza kundi la Hamas kukubali mpango wa usitishwaji mapigano uliopendekezwa na Israel. Kwa upande wake, waziri wa mambo ya nje wa Misri amesema Hamas wamekubali mpango huo wa amani.

Blinken ambaye alizungumza kwa simu na waziri wa ulinzi wa Israel, Yoav Gallant amesema kunamatumaini ya kufikia makubaliano. Lakini ofisi ya Gallant imesema waziri huyo amemuambia Blinken kwamba mpango wowote wa kumaliza vita lalizima ujumuishe kusambaratishwa kwa kundi la Hamas na kukomesha uongozi wake Gaza.

Huku hayo yakijiri, Rais wa Chile Gabriel Boric amesema nchi yake inaungana na Afrika Kusini dhidi ya Israel katika kesi yake katika Mahakama ya Kimataifa ya Haki, ICJ. Akihutubia bunge la nchi yake mwishoni mwa wiki, Boric alishutumu hali mbaya ya kibinadamu huko Gaza na kutoa wito wa majibu madhubuti kutoka kwa jumuiya ya kimataifa.

 

Vyanzo : AFP, Reuters, DPA