1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Yanga ya Tanzania yacharazwa 2-1 na Augsburg ya Ujerumani

20 Julai 2024

Mabingwa wa Ligi kuu kandanda ya Tanzania, Klabu ya soka ya Yanga wamemenyana na timu ya soka ya Augsburg ya Ujerumani katika mashindano ya Mpumalanga yanayoendelea huko Afrika ya Kusini

https://p.dw.com/p/4iXeC
Fußball | Bundesliga | FC Augsburg vs 1. FC Heidenheim 1846
Picha: Sebastian Widmann/Getty Images

Katika mchezo huo timu ya Augsburg inayoshiriki ligi ya kandanda ya Ujerumani, Bundesligaimeinyuka Yanga  magoli 2-1.

Augsburg ilikuwa ya kwanza kuliona lango la Yanga katika dakika 36 ya mchezo kupitia kwa nyota wake mholanzi Mads Valentin Pedersen.

Dakika za kipindi cha kwanza katika mchezo huo uliokuwa wa vuta nikivute ulishuhudia golikipa wa Yanga Djigui Diarra, akifanya kazi ya zaida kuokoa michomo ya washambuliaji wa Augsburg waliokuwa wakilisakama lango lake.

Young Africans
Mchezaji Nyota wa Yanga Aziz Ki, mwenye jezi namaba 10 na wenzake Picha: Young Africans

Hadi kipindi cha kwanza kinakamilika matokeo yalibaki vilevile Augsburg wakiwa kifua mbele kwa goli moja.

Dakika 45 za kipindi cha pili.

Kipindi cha pili kati ya timu ya Ujerumani Augsburg na mabingwa wa Tanzania Young African, Yanga walianza kwa kasi kutaka kusawazisha goli lakini umakini wa vijana wa Ujerumani uliendelea kuwaweka mbele ya mchezo.

Dakika ya 79 ya mchezo, Augsburg wakaijapatia goli la pili na la ushindi kupitia kwa nyota wake Philip Tietz.

Soma Pia:Azam yathibitisha kujiengua kwa Kagame Cup 

Baada ya Augsburg kupata goli hilo la pili Yanga ni kama vile waliamka mchezoni na kuanza kulishambulia lango la wapinzani wao, jitihada hizo zilizaa matunda dakika ya 84 ya mchezo baada ya mchezaji wake mpya Jean Baleke kuutia mpira wavuni na kuyafanya matokeo kuwa 2-1.

Waliokuwa Simba sasa wako Yanga.

Katika mchezo huu wa michunao ya Mpumalanga aliyekuwa nyota wa klabu ya Simba, Clotous Chota Chama kwa mara ya kwanza ameshuhudiwa uwanjani akiwa na jezi ya wanajangwani ikiwa ni siku chache tu tangu amalizane na timu yake ya zamani ya wekundu wa msimbazi Simba.

Young Africans
Wachezaji wa Yanga kushoto mwenye jezi namba 25 ni Musonda. Katikati aliyeinama ni Aziz Ki na kulia ni Pacome Zouzou.Picha: Young Africans

Mbali na Chama, Nyota mwingine aliyeywahi kukipiga kwenye timu ya Simba msimu uliopita Jean Baleke na aliyefunga goli pekee la kufutia machozi kwa Yanga ameonekana akiwa na uzi wa Yanga baada ya tetesi za wiki kadhaa za kuhusishwa na timu hiyo yenye maskani yake jijini Dar es Salaam.

Kwa sasa klabu ya Yanga iko nchini Afrika ya Kusini kushiriki michuano ya Mpumalanga pamoja na timu zingine kama TS Galaxy ya Afrika Kusini, Augsburg ya Ujerumani na Mbabane Swallow FC ya Eswatini.