1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUganda

Wanafunzi 3 kati ya 6 waliotekwa nyara Uganda watoroka

21 Juni 2023

Wanafunzi 3 kati ya 6 waliotekwa nyara kwenye shule ya bweni magharibi mwa Uganda wamefaulu kutoroka na kujiwasilisha kwa jeshi la Uganda. Wakati huohuo wanajeshi wa Uganda na wa DRC wanaendelea kuwasaka wavamizi hao

https://p.dw.com/p/4SsiD
Mpondwe Massaker auf Schule / Uganada
Picha: Hajarah Nalwadda/ASSOCIATED PRESS/picture alliance

Familia za wanafunzi watatu ambao wameweza kuwaponyoka watekaji wao zina furaha kubwa ila wale ambao watoto wao wangali hawajulikani waliko wapo katika majonzi. Msemaji wa jeshi la Uganda brigedia Felix Kulayigye ameiambia DW kwamba wanafanya kila juhudi kuwafuatilia mateka hao .

Wanafunzi manusura wanaendelea kupata matibabu

Wakati huohuo, wanafunzi manusura wa kisa hicho wanaendelea kupata matibabu katika hospitali kuu ya wilaya ya Kasese huku wakisimulia jinsi walivyonusurika. 

Uganda Trauer nach Rebellen Attacke auf Schüler
Mwili wa mhanga mmoja wa shambulizi la shule ya upili ya Lhubiriha azikwaPicha: Hajarah Nalwadda/AP Photo/picture alliance

Hapo awali palikuwa na wazo kuwa wavamizi hao walikuwa genge lililokodishwa kufanya mauaji hao kutokana na mvutano wa umiliki wa shule hiyo. Lakini msemaji wa jeshi amefahamisha kuwa sasa wamethibitisha wavamizi hao ni wa kundi la waasi wa ADF ambao huvamia na kuwauwa raia katika nchi ya Congo.

Vikosi zaidi vyatumwa Kasese

Msemaji huyo ameongeza kuwa wametuma vikosi zaidi vya wanajeshi eneo la Kasese kuwahakikishia wananchi usalama dhidi ya visa vya uvamizi. Hii leo, waziri wa ulinzi anatarajiwa kuwasilisha taarifa rasmi katika bunge la Uganda kuhusu kisa hicho. Kwingineko, mwanamume mmoja aliyesambaza habari kwenye jukwaa la kijamii la Tik Tok akidai kuwa alikuwa miongoni mwa kundi la ADF lililofanya shambulizi hilo la kikatili lililowauwa watu 42 amekamatwa na polisi.