1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUganda

Wabunge wawili wa upinzani NUP warudi bungeni Uganda

4 Aprili 2023

Wabunge wawili wa chama kikuu cha upinzani nchini Uganda cha NUP wamerudi bungeni baada ya kuwa gerezani kwa muda wa takriban miaka miwili. Hata hivyo, wanaendelea kukabiliwa na mashtaka ya wimbi la mauaji

https://p.dw.com/p/4PgnL
Uganda führt drakonisches Anti-Schwulengesetz ein
Picha: Abubaker Lubowa/REUTERS

Hata hivyo, waheshimiwa hao ambao waliachiwa kwa dhamana wanaendelea kukabiliwa na mashtaka ya wimbi la mauaji lililokumba kanda ya kusini mwa nchi hiyo kati ya mwaka 2020 na 2021.

Wabunge Allan SSewanyana na Mohamad SSegirinya wamepokelewa kwa furaha  kwenye majengo ya bunge hususan na wenzao wa upinzani. Hawakuweza kuwawakilisha wakazi kutoka divisheni mbili kuu za mji mkuu wa Kampala za Kawempe na Makindye katika muda wa miaka miwili hivi tangu walipokamatwa mwaka mwezi Septemba mwaka 2021. Ila kutokana na utaratibu wa bunge, hawakupoteza viti vyao kwani walikuwa rumande.

Soma pia: Museveni aapishwa kwa muhula wa sita madarakani

Hatai hivyo, naibu spika alimkata kilimi kiranja wa upinzani aliyetaka wabunge hao wapewe fursa kutoa hotuba fupi bungeni akisema kuwa hoja hiyo haikuwa kwenye ratiba ya siku. Lakini aliahidi kuwapa fursa wanayostahili kama wabunge licha ya kuwa bado wanakabiliwa na mashtaka ya mauaji. 

Robert Kyagulanyi kiongozi wa NUP Uganda
Chama cha upinzani Uganda cha NUP kinaongozwa na Robert Kyagulanyi maarufu kama Bobby WinePicha: Emmanuel Lubega/DW

Mapema kabla ya kuingia ndani ya ukumbi wa bunge, wabunge hao walisimulia  masaibu yao wakiwa gerezani. Waliezelea jinsi walivyougua magonjwa mbalimbali na wamechukua muda wa siku 39 tangu walipoachiwa kupata nafuu. Wameapa kuendelea na harakati zao za kupigania haki za binadamu na uhuru  wa raia pamoja na ulaji rushwa. Rais Museveni amekuwa akisisitiza kuwa washukiwa wa kesi za mauaji na ubakaji wasiachiwe kwa dhamana na hii ni mojawapo ya hali zinazoweka kitengo cha kisheria katika mashaka katika kufanya maamuzi ya kuwachia kwa dhamana. Mbunge Sewanyana amemkosoa rais kwa kujaribu kuikiuka katiba ya nchi kuhusiana na haki za washukiwa kuachiwa kwa dhamana. amesema

Soma pia: Bobi Wine asema yuko chini ya ´kizuizi cha nyumbani´

Wabunge sewanyana na segirinya wamekanusha madai kuwa hatua ya kuachiwa kwao ilitokana na maafikiano kati ya serikali na upinzani. walipoachiwa mara ya kwanza walikamatwa nje ya gereza na kuburutwa na askari wa vyombo ya vya usalama na kurudishwa mahakamani ambako walifunguliwa mashtaka mengine. Kwingineko, wafuasi 28 wa chama cha NUP wamenyimwa dhamana baada ya kushindwa kuwasilisha wadhamini wanaostahili. Wenzao wanne wameweza kuachiwa baada ya mahakama kuwakubali mwadhamini wao. Wafuasi hao wamekuwa kizuizini tangu mwaka 2020 walipokamatwa kuhusiana na vurugu za kisiasa kuelekea uchaguzi mkuu.

Lubega Emmanuel DW Kampala.