1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUrusi

Prigozhin miongoni mwa waliokufa ajali ya ndege Urusi

24 Agosti 2023

Duru nchini Urusi zinasema kiongozi wa Kundi la Mamluki wa Kirusi la Wagner, Yevgeny Prigozhin, amefariki dunia baada ya ndege inayoaminika alikuwemo kuanguka na kuteketea kwa moto hapo jana jioni.

https://p.dw.com/p/4VWFj
Yevgeny Prigozhin
Yevgeny PrigozhinPicha: PMC Wagner/Telegram/REUTERS

Ukurasa wa mtandao wa Telegram wenye jina la, Grey Zone, ambao una mafungamano na Kundi la Wagner, umeripoti taarifa za kifo cha Prigozhin saa chache baada ya ajali hiyo ya ndege kutokea.

Wakala wa Usafiri wa Anga nchini Urusi nao umechapisha orodha ya majina ya watu 10 waliokuwemo kwenye ndege hiyo ikiwemo jina la Yevgeny Prigozhin, na inaarifiwa wote wamepoteza maisha.

Ndege hiyo aina ya Embraer iliyokuwa njiani kutoka mjini Moscow kuelekea St. Petersburg, ilianguka katika kijiji kimoja kilichopo kwenye mkoa wa Tver.Prigozhin aligonga vichwa vya habari duniani baada ya kuongoza uasi uliodumu kwa muda mfupi dhidi ya mamlaka za Urusi mnamo Juni 23 hadi 24. Uasi huo wa Wagner ulisitishwa kwa makubaliano yaliyoshuhudia Prigozhin akiridhia kuihama Urusi na kwenda taifa jirani la Belarus.