1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaNigeria

Viongozi wa ECOWAS wawaonya viongozi wa mapinduzi, Niger

30 Julai 2023

Viongozi wa Jumuiya ya Maendeleo Magharibi mwa Afrika, ECOWAS wamekubaliana kuiwekea vikwazo vya kifedha na kusafiri viongozi wa kijeshi walioongoza mapinduzi nchini Niger yaliyomuondoa rais Mohamed Bazoum.

https://p.dw.com/p/4UZ0t
Niger Niamey | Proteste | Unterstützung der Militärputschisten
Wafuasi wa kiongozi wa mapinduzi nchini Niger Jenerali Abdourahamane Tiani, wakiandamana katika mji mkuu Niamey.Picha: AFP/Getty Images

Viongozi hao waliokutana katika mkutano wa kilele usio wa kawaida kuijadili Niger aidha wameupa wiki moja utawala huo wa kijeshi kuachia madaraka, na kuwaonya kwamba hawaondoi uwezekano wa kutumia nguvu.

Awali, waandamanaji wanaounga mkono utawala huo walivamia ubalozi wa Ufaransa nchini Niger, wakichana bendera za Ufaransa na kuzipandisha za Niger na Urusi, huku wakisikika kuisifu Urusi na rais Vladimir Putin.

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amelaani hatua hiyo na kusema shambulizi lolote dhidi ya raia ama maslahi yake nchini Niger litaisukuma kuchukua hatua kali na za haraka, baada ya hapo jana kutangaza kuondoa misaada yote ya maendeleo nchini Niger na kutaka rais aliyeondolewa kurejeshwa madarakani.