1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
Ugaidi

UN: Machafuko yasambaa hadi maeneo ya vijijini Haiti

29 Novemba 2023

Umoja wa Mataifa umesema vita baina ya makundi ya uhalifu nchini Haiti hivi sasa vinasambaa kutokea mji mkuu Port au Prince hadi kwenye maeneo ya mashambani na kusababisha maelfu ya wakazi kukimbia makazi yao.

https://p.dw.com/p/4ZZOM
Sicherheit in Haiti
Picha: Rodrigo Abd/AP Photo/picture alliance

Umoja wa Mataifa umesema vita baina ya makundi ya uhalifu nchini Haiti hivi sasa vinasambaa kutokea mji mkuu Port au Prince hadi kwenye maeneo ya mashambani na kusababisha maelfu ya wakazi kukimbia makazi yao na kusabisha athari kubwa katika upatikanaji wa vyakula muhimu.

Machafuko hayo sasa yamesambaa hadi kwenye mkoa wa Bas-Artibonite, kaskazini mwa mji mkuu ambako ndiko kunakozalishwa vyakula kwa wingi kama mchele.

Soma pia: Bunge la Kenya yaidhinisha polisi kutumwa nchini Haiti

Umoja wa Mataifa umesema watu 22,000 wamekimbia makwao kutokana na visa vya mauaji, uporaji, utekaji na kuongezeka kwa matukio ya unyanyasaji wa kijinsia.

Kamishna mkuu wa haki za binaadamu wa Umoja wa Mataifa, Volker Turk amesema hali nchini Haiti ni mbaya sana akiongeza kuwa kikosi kinachoungwa mkono na Umoja wa Mataifa kinapaswa kupelekwa Haiti haraka iwezekanavyo.

Kikosi cha kimataifa kikiongozwa na Kenya, kimepewa ridhaa, lakini huenda ikachukua miezi kadhaa ili kupelekwa Haiti.