1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yaisaidia Afrika Mashariki katika mambo muhimu

9 Novemba 2021

Jumuiya ya Afrika Mashariki na Ujerumani zimetia saini mwafaka wa makubaliano wenye thamani ya dola milioni 35 katika nyanja za raslimali za maji, utangamano wa kiuchumi na utayarifu wa majanga.

https://p.dw.com/p/42lHo
Deutschland Tansania Vertragsunterzeichnung in Arusha
Picha: Deutsche Botschaft,Tansania

Akizungumza wakati wa kutia saini  makubaliano hayo katika makao makuu ya Umoja huo yaliyoko Arusha, Tanzania, Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo Balozi Daktari Peter Mathuki amesema, mchango huo utasaidia  pakubwa kuleta ubora na usalama wa maji katika ziwa Victoria  na jumuiya nzima ya Afrika Mashariki. 

Mradi wa kwanza wa kiufundi wenye thamani ya dola milioni 3.8 za Marekani utazinduliwa mapema Januari mwakani na unalenga kuboresha Tume ya Ziwa Victoria ili kuweza kuafikia malengo ya ikiwa ni pamoja na kusimamia raslimali za maji, na pia kuboresha huduma zake.

Mradi wa pili unakadiriwa kupindukia milioni 17.3

Mradi wa pili wa ushirikiano unakisiwa kuwa wa thamani ya dola milioni 17.3, huku ukilenga kuimarisha ushirikiano wa kiuchumi kati ya mataifa ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Eneo la Ziwa Victoria, tayari linatoa mapato ya asilimia 40 ya pato lote la jumla ya mataifa yaliyoko kwenye jumuiya ya afrika mashariki huku watu milioni 40 wanaoishi karibu nalo wakilitegemea. Daktari Peter Muthuki ni Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Deutschland Tansania Vertragsunterzeichnung in Arusha
Balazi wa Ujerumani nchini Tanzania, Regine Hess na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki, Peter MathukiPicha: Deutsche Botschaft,Tansania

Mradi wa tatu wa ushirikiano kati ya Jumuiya ya Afrika Mashariki na Ujerumani unakisiwa kuwa wenye thamani ya dola milioni 13.9. Mradi huu unalenga kupanua ushirikiano uliopo kati ya Ujerumani na Jumuiya ya Afrika Mashariki wa kukabiliana na majanga na hata kuimarisha asasi za kuyadhibiti majanga hayo.

Uhusianoa kati ya Ujerumani na Afrika Mashariki utasaidia kupunguza changamoto

Balozi wa Ujerumani, nchini Tanzania, Regine Hess amesema kuwa kuboreshwa kwa mahusiano kati ya Ujerumani na Jumuiya ya Afrika Mashariki, huku akitilia mkazo maabara, kutasaidia Jumuiya kukabiliana na majanga na changamoto za kiafya siku zijazo.

Daktari Mathuki alipongeza Ujerumani kwa juhudi zake za ushirikiano pamoja na mchango wake wa kuboresha utangamano katika jumuiya ya afrika mashariki. Aliongeza kusema kuwa kwa kipindi cha miaka 20, Ujerumani imekuwa ikitoa mchango wake kwa juhudi za kufanikisha malengo ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Ujerumani imesambaza maabara kwa mataifa washirika wa jumuiya ya Afrika Mashariki ambayo yanasaidia kukabiliana na janga la UVIKO. Kwa sasa sampuli 560000 zimepimwa huku wafanyikazi 103 wakifunzwwa kukusanya data na pia kuwapima wagonjwa wa virusi vya UVIKO. Maambukizi ya ugonjwa huo yanazidi kupungua siku zinavyosonga.

Chanzo: DW, Nairobi