1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ujerumani yaendelea kuinyima silaha Saudi Arabia

24 Machi 2020

Mgogoro wa muda mrefu nchini Yemen hauonyeshi dalili za kumalizika. Watu wanaendelea kuuawa na wengine wanateseka. Umoja wa Mataifa umesema mgogoro huo ndio mbaya kabisa kuwahi kutokea kwa sasa duniani.

https://p.dw.com/p/3ZxHr
Deutschland Hafen von Mukran | Küstenschutzboot für Saudi-Arabien
Picha: picture-alliance/dpa/S. Sauer

Mgogoro huo unaoelezewa kuwa ni vita vya kiwakala kati ya majeshi ya serikali ya Yemen yanayoungwa mkono na Saudi Arabia yanayopambana na waasi wa Kihouthi wanaoungwa mkono na Iran umesababisha hali mbaya nchini humo. Kutokana na hali hiyo asilimia 80 ya wananchi wapatao milioni 24 sasa wanategemea misaada ya kimataifa.

Mjumbe maalum wa Umoja wa Mataifa anayeshughulikia mgogoro wa Yemen Martin Griffiths amesema uwezekano wa nchi kadhaa kuhusika moja kwa moja kwenye mgogoro huo umezidi kuwa mkubwa.

Deutschland Rüstungsexporte Patrouillenboote für Saudi-Arabien
Boti ya doria ya Suadi Arabia iliyotengenezwa nchini Ujerumani ikiendelea na matengnezo mwaka 2018, kabla ya serikali kusitisha mauzo ya silaha kwa Saudi Arabia.Picha: picture-alliance/dpa/S. Sauer

Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch limetilia maanani mashambulio ya anga yanayofanywa na vikosi vinavyoongozwa na Saudi Arabia yanayosababisha vifo vya maalfu ya watu na sehemu nyingi za kiraia. Asasi hiyo ya hali za binadamu imesema mashambulio hayo yanakiuka sheria za kimataifa kuhusu vita.

Maafa makubwa kwa watoto

Wakati huo huo shirika la kutetea haki za watoto Save the Children limesema vita vya nchini Yemen vimesababisha maafa makubwa kwa watoto hasa afya yao ya kiakili. Majeshi ya serikali ya Yemen yanayoungwa mkono na mfungamano wa kijeshi unaoongozwa na Saudi Arabia yamekuwa yanapambana na waasi wa Kihouthi wanaoungwa mkono na Iran kwa muda wa zaidi ya miaka mitano na mpaka sasa hakuna dalili ya mgogoro huo kumalizika.

Jemen Konflikt Saudi Arabien
Wanajeshi wa Saudi Arabia wakitoa ulinzi kabla ya kushusha kwa misaada kutoka ndege ya Saudi Arabia katika mkoa wa kati wa Marib nchini Yemen, Machi, 12, 2018.Picha: Getty Images/A. Al-Qadry

Na katika juhudi za kimataifa za kujaribu kuutatua mgogoro huo serikali ya Ujerumani imesimamisha kupeleka silaha kwenye nchi zinazohusika katika mgogoro wa Yemen. Uamuzi huo umeafikiwa na vyama vinavyoongoza serikali na hatua hiyo itaihusu Saudi Arabia mnunuzi mkuu wa silaha kutoka Ujerumani.

Uamuzi huo utaanza kutekelezwa mara moja. Umoja wa mataifa umezilaumu pande zote zinazohusika katika mgogoro huo kwa kukikuka haki za binadamu na kwamba pande hizo zinaweza kukabiliwa na mashtaka ya uhalifu wa kivita.

Vyanzo; AFP, DW