1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

AfD yatafuta uungwaji mkono katika chaguzi Saxony, Thuringia

1 Septemba 2024

Majimbo mawili ya mashariki mwa Ujerumani,Thuringia na Saxony yanapiga kura leo Jumapili katika uchaguzi muhumi unaoweza kuonesha mustakabali wa kisiasa wa nchi hii.

https://p.dw.com/p/4k99J
Uchaguzi wa jimbo Thuringia · Kituo cha kupigia kura
Mpiga kura anaweka karatasi ya kupigia kura kwenye sanduku la kura kwenye kituo cha kupigia kura katikati mwa mji wa Erfurt. Picha: Martin Schutt/dpa/picture alliance

Vituo vya kupiga kura vilifunguliwa saa mbili asubuhi kwa saa za Ujerumani na vinatarajiwa kufungwa saa kumi na mbili jioni.Uchaguzi huo wa bunge wa majimbo huenda ukaonesha mwelekeo wa mitazamo ya Wajerumani kisiasa katika uchaguzi mkuu ujao kitaifa.

Kwa kiasi kikubwa kinachotazamwa ni kwa namna gani chama cha siasa kali za mrengo wa kulia cha AfD ambacho huenda kinaweza kuwa chama chenye nguvu katika uchaguzi wa majimbo kwa mara ya kwanza,kitaungwa mkono kwenye uchaguzi huu.

Ishara ya kupoteza umaarufu kwa vyama vilivyo katika serikali ya mseto

Uchaguzi wa jimbo Thuringia · Kituo cha kupigia kura
Wapiga kura walipiga kura zao katika kituo cha kupigia kura katikati mwa jiji la Erfurt. Picha: Martin Schutt/dpa/picture alliance

Inaonesha kwamba vyama vitatu vilivyomo kwenye serikali ya mseto inayopoteza umaarufu kitaifa inayoongozwa na Kansela Olaf Scholz inaelekea kupata matokeo mabaya zaidi katika uchaguzi huu wa majimbo na huenda matokeo hayo yakazidi kuleta migawanyiko miongoni mwa viongozi hao wakati ukiwa umebakia mwaka mmoja tu ufanyike uchaguzi wa bunge kitaifa.

Uchaguzi mkuu wa bunge nchini Ujerumani utafanyika mwezi Septemba mwaka 2025. Kabla ya uchaguzi huu wa Thuringia na Saxony,zilifanyika kura za maoni hivi karibuni ambazo zimeonesha chama cha AfDkitapata ushindi wa wazi katika jimbo la Thuringia na karibu na chama cha siasa za wastani za mrengo wa kulia cha Christian Democratic CDU.

Shirika la ujasusi nchini Ujerumani,limekiorodhesha chama cha AfD katika majimbo ya Thuringia na Saxony kuwa chama cha itikadi kali za mrengo wa kulia na limekuwa likikichunguza chama hicho kama kundi linaloshukiwa kuwa la itikadi kali kote katika jimbo la Brandenburng na ngazi ya kitaifa.

Soma zaidi:Wajerumani weusi wahofia ushindi wa AFD majimbo ya mashariki

Kiongozi wa chama hicho katika jimbo la Thuringia, Björn Höcke aliyekuwa mwalimu wa historia alikutwa na hatia mara mbili mwaka huu kwa kutumia nembo ya Manazi iliyopigwa marufuku na alipigwa faini.Na bado anakabiliwa na kesi nyingine ya kuhusishwa na uchochezi.

 

DW Kiswahili | Saumu Mwasimba
Saumu Mwasimba Mhariri na mtangazaji wa Idhaa ya Kiswahili ya DW