1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ufaransa yajidhatiti kiusalama kuelekea Olimpiki?

Hawa Bihoga
22 Julai 2024

Kuelekea michuano ya Olimpiki ya mjini Paris itakayoanza kutimua vumbi baadae mwezi huu idara ya usalama nchini Ufaransa, imejikita katika kushughulikia eneo lisilo la kawaida la kijajusi kuzuia mashambulio yakigaidi.

https://p.dw.com/p/4iabF
Paris, Ufaransa | Nembo ya Michuono ya Olimpiki
Nembo ya Michuono ya OlimpikiPicha: IMAGO/ABACAPRESS

Ufaransa inachukua hatua hii kufuatia mashambulizi mawili makubwa yaliofanyika mwaka huu ambapo mamlaka inasema, yalifanywa na wanachama wa ISIS-K ambao wanamafungamano na kundi la dola la Kiislam kwenye tawi lililofufuliwa hivi karibuni na kupewa jina la kihistoria la Khorasan ambalo lilijumuisha sehemu ya Iran, Afghanistan na Asia ya Kati.

Miongoni mwa matukio hayo ni pamoja na shambulio la kujitoa muhanga mara mbili nchini Iran mnamo Januari 3 liliua takriban watu 100 katika hafla ya kumbukumbu ya kamanda wa Walinzi wa Mapinduzi aliyeuawa Qassem Soleimani, wakati mkasa wa Moscow mnamo Machi 22 ulishuhudia watu wenye silaha wakiwafyatulia risasi watu waliohudhuria tamasha katika Ukumbi wa Crocus City, na kuua zaidi ya watu 130.

Mamlaka nchini Ufaransa inasema tayari imekwishazuia shambulio moja ambalo limehusishwa na itikadi kali kwenye michezo ya Olimpiki.

Kufuatia mkasa huo kijana mmoja anaeshukiwa kupanga njama ya kujitoa muhanga kwa niaba ya kundi la dola la kiislam katika uwanja wa mpira wa Saint-Etienne, ambapo Ufaransa, Marekani na Ukraine zitacheza, alikamatwa.

Soma pia:Waandalizi wa Olimpiki Paris wasema wako tayari kwa Michezo

Vyombo vya habari nchini humo vilimnukuu Waziri wa Mambo ya Ndani  Gerald Darmanin alisema hakuna kitisho chochocte cha moja kwa moja kuhusu mashambulizi ya kigaidi, na kwamba wamejiandaa vilivyo katika kuhakikisha kuwa usalama unashuhudiwa katika michezo hiyo ya Olimpiki ambayo hufanyika kila mwaka.

"Hakuna kitisho chochote katika sherehe za ufunguzi wa michezo ya Olimpiki, lakini tupo makini." Alisema Waziri huyo.

Aidha aliongeza kwamba "katika eneo la Alsace tumemkama mtu mmoja mfuasi wa siasa za mrengo mkali wa kulia ambaye alikuwa akichochea, namnukuu. Alisema mashambulio na vurugu kupinga Michezo ya Olimpiki."

Kwanini Ufaransa inalengwa na aina hiyo ya mashambulizi?

Pamoja na historia yake ya ukoloni, hisia za kupinga Uislamu na ushiriki wa kihistoria katika vita vya Mashariki ya Kati na Afrika, Ufaransa imekuwa ikilengwa kwa muda mrefu na mashambulio yanayohusishwa na itikadi kali.

Ufaransa kupiga marufuku abaya katika shule za serikali

Mwezi uliopita Mkuu wa polisi katika mji wa Paris Laurent Nunuez alisema kwamba mashambulio ya kiitikadi kali yameendelea kusalia kuwa kitisho kikuu katika mashindano ya Olimpiki, licha ya mamlakakusema hakuna kitisho cha moja kwa moja dhidi ya michuano hiyo.

Tajikistan, iliyokumbwa na vita vya wenyewe kwa wenyewe katika miaka ya 1990, ndiyo nchi maskini zaidi ya jamhuri ya zamani ya Soviet na inategemea fedha kutoka kwa wahamiaji - haswa nchini Urusi - kwa karibu nusu ya pato lake la kiuchumi.

Baadhi ya wataalamu wa masuala ya usala a wanasema vijana maskini, waliotengwa wanaoishi nje ya nchi ya Tajikistan wamethibitisha kuvutiwa na kundi la ISIS-K na kujiunga.

Soma pia:Makundi ya Haki za Olimpiki yamsihi rais wa IOC kuondoa marufuku ya hijab

Chanzo kimoja cha kijasusi nchini Ufaransa ambacho hakikutaka jina lake linatajwe  alisema kwamba kundi la ISIS-K linatowa tishio jipya, akiutaja kama ushahidi alizungumzia kisa cha raia mmoja wa Tajikistan ambae alikamatwa mnamo 2022 kwa kupanga shambulio huko Strasbourg, chanzo hicho kilisema mtu huyo alöikuwa akifanya kazi chini ya kundi hilo.

Hata hivyo jasusi wa zamani wa Marekani ambae hakutana jina lake litajwe alisema kwamba  idara ya usalama Ufaransa ipo imara, lakini kuendelea kushinikiza kupata taarifa kutoka katika makundi ya itikadi kali ya Tajikistan kunaweza kusababisha madhara kwa kuendeleza harakati zao kwa uangalifu wa hali ya juu.