1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ufaransa, England zapigiwa upatu kubeba Euro 2024

6 Juni 2024

Maandalizi yanaendelea kuelekea michuano ya Kombe la Mataifa ya Ulaya EURO 2024 itakayotifua vumbi kuanzia Juni 14 hapa Ujerumani.

https://p.dw.com/p/4gj5z
Timu ya taifa ya kandanda ya Ujerumani
Wenyeji Ujerumani wanakabiliwa na shinikizo la kupata matokeo bora katika mashindano ya Euro 2024Picha: Alexander Hassenstein/Getty Images

Hata hivyo, timu tatu ndio zinazopigiwa upatu kutawazwa masogora wa kandanda barani Ulaya nazo ni Ufaransa, Uingereza na wenyeji Ujerumani. 

Maandalizi ya mashindano haya ya mwezi mzima ni muhimu ukizingatia jinsi mashindano yaliyofanyika miaka mitatu iliyopita yalivyokuwa, kimya kimya kutokana na janga la Uviko-19 na yalichezwa kote barani Ulaya badala ya kuandaliwa na taifa moja na idadi ndogo ya mashabiki ndio waliokubaliwa kuingia uwanjani.

Soma pia: Toni Kroos kutundika daluga baada ya EURO 2024

Wakati huu mashabiki wote watashuka katika viwanja kumi vya Ujerumani, wengi wakiwa na kumbukumbu za mwaka usiosahaulika wa 2006 ambao ndio ulikuwa wa mwisho Ujerumani kuwa mwandalizi wa mashindano makuu.

Mshambuliaji Mbappe
Kylian Mbappe ni atakiongoza kikosi cha Ufaransa ambacho kilimaliza makamu bingwa Kombe la DuniaPicha: Tnani Badreddine/DeFodi Images/picture alliance

Katika mashindano ya mwaka 2006, Ujerumani ilifika hatua ya nusu fainali licha ya maswali kuibuka kabla kuanza kwa mashindano yenyewe kuhusiana na uwezo wa timu ya taifa ya Die Mannshcaft.

Safari hii, kuna gumzo sawia na hilo ukizingatia kwamba Ujerumani imeondolewa kutoka kwenye mashindano mawili yaliyopita ya Kombe la Dunia mara mbili katika hatua ya makundi na mashindano ya Euro yaliyopita waliyaaga mashindano hayo katika hatua ya mtoano ya 16 bora.

Soma pia: EURO 2024: Kikosi cha Uholanzi

Lakini utakuwa ujuha kusema kwamba Ujerumani hawana nafasi ya kulishinda kombe hilo mwaka huu ukizingatia wacheza walio nao. Kocha wao Julian Nagelsmann anasema anahisi kwamba wanaweza kulishinda taji hilo.

Timu ya taifa ya England
England ilipoteza kwa Italia katika mashindano ya mwaka wa 2020 katika dimba la Wembley mjini LondonPicha: Matt Impey/Shutterstock/IMAGO

Ila kuna Ufaransa na England, timu mbili ambazo zinapigiwa upatu na wengi kuwa zinaweza kuibuka na ubingwa. Ufaransa ndiyo timu ya Ulaya inayoorodheshwa juu zaidi katika orodha ya shirikisho la kandanda duniani FIFA ya timu bora na imetinga fainali mbili zilizopita za Kombe la Dunia, ikishinda fainali moja na kupoteza moja.

Timu hiii ina hamu sana ya kushinda taji lao la kwanza la Ulaya tangu mwaka 2000 walipokuwa wachezaji kama kina Zinedine Zidane na Thierry Henry. Safari hii lakini mbali na nyota wao Kylian Mbappe, kuna wachezaji wengi kwenye kikosi chao walio na uzoefu na ubora wa hali ya juu.

UEFA EURO 2024
Ujerumani imekamilisha mipango ya kuandaa tamasha maarufu kabisa la kandanda msimu wa kiangaziPicha: ABB/picture alliance

England kwa upande wao, wanaingia kwenye mashindano hayo wakifahamu kwamba hawajayashinda kwani mashindano yaliyopita mwaka 2021 waliipoteza fainali kwa mikwaju ya penalti mikononi mwa Italia. Na katika Kombe la Dunia lililopita huko Qatar, walifungwa na Ufaransa katika robo fainali.

Lakini katika mashindano haya, wana wachezaji ambao wanaweza kuwategemea pakubwa, Harry Kane na Jude Bellingham. Wote hawa wanaifahamu Ujerumani vyema, Kane akiwa ndiye mfungaji bora wa Ligi Kuu ya Ujerumani, Bundesliga na Bellingham ambaye kwa sasa yuko Real Madrid, aliwahi kucheza katika klabu ya Ujerumani ya Borussia Dortmund.