1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ubaguzi: Watu Weusi waathirika hasa nchini Ujerumani

8 Novemba 2023

Watu weusi, Waasia na Waislamu wamefichua kiwango cha ubaguzi wanaopitia nchini Ujerumani kila siku, katika ripoti mpya ya ufuatiliaji wa ubaguzi kitaifa. Watu weupe pia wameripoti kubaguliwa kiumri na kijinsia.

https://p.dw.com/p/4Ya8X
Symbolfoto Antidiskriminierungsgesetz I Antidiskriminierung I Antirassismus
Ubaguzi wa rangi na mwingine ni matukio ya kila siku kwa watu wasio weupe nchini UjerumaniPicha: Christoph Soeder/dpa/picture alliance

Sura za kudharauliana au matusi ni matukio ya kila siku nchini Ujerumani kwa watu wenye ngozi nyeusi, wanawake wa Kiislamu wanaovaa hijabu na wanaozungumza Kijerumani vibaya au kutozungumza kabisa. Ubaguzi nchini Ujerumani una sura nyingi mbaya na umeenea katika jamii nzima.
Matokeo hayo siyo mapya wala ya kushangaza kabisa lakini ni mara chache yamebainishwa kwa usahihi kama ilivyo katika ripoti ya Uchunguzi wa Kitaifa wa Ubaguzi ya Kituo cha Ujerumani cha Utafiti wa Ushirikishwaji na Uhamiaji (DeZIM), ambayo iliwasilishwa kwa serikali Berlin Novemba. 7. Takriban watu 21,000 walifanyiwa utafiti kuanzia Juni hadi Novemba 2022.

Ubaguzi Ujerumani ni maisha ya kila siku

Kulingana na ripoti ya utafiti huo, zaidi ya nusu ya watu Weusi nchini Ujerumani, sawa na asilimia 54, wamekumbana na ubaguzi wa rangi angalau mara moja. Takriban mwanamke mmoja kati ya watano kutoka kundi hili la watu walisema walitishwa au kunyanyaswa mara kadhaa kwa mwaka. Miongoni mwa waliohojiwa, asilimia 14 ya wanawake wa Kiislamu na asilimia 13 ya wanawake wa Asia waliripoti matatizo kama hayo.

Ujerumani| Maandamano ya kupinga ubaguzi
Watu weusi, Waasia na Waislamu wanaeleza kupitia aina nyingi za ubaguzi kila siku.Picha: Christoph Soeder/dpa/picture alliance

Soma pia: Utafiti: Ubaguzi dhidi ya watu weusi bado upo Ulaya

"Matukio ya mara kwa mara ya ubaguzi na ubaguzi wa rangi yana madhara kwa afya na yanahusishwa na kupoteza imani katika taasisi za serikali - hii inaweza kudhoofisha na kutishia demokrasia," alisema Mkurugenzi wa DeZIM Naika Foroutan, ambaye anataka kuanzishwa mfumo wa kudumu wa ufuatiliaji nchini Ujerumani.

Asilimia 41 ya wanaume Weusi na asilimia 39 ya wanaume Waislamu waliripoti kuwa wamekumbana na ubaguzi wa rangi walipokuwa wakishughulika na polisi, huku makundi haya yakielezea pia kukumbwa na ubaguzi wa katika ofisi za umma.

Pia wanapitia ubaguzi wa rangi linapokuja suala la afya. Watu wasio weupe wana shida zaidi kupata miadi kwa daktari na wana uwezekano mdogo wa kuhisi shida zao zinachukuliwa kwa uzito. Watu Weusi, Waislamu na Waasia walioshiriki utafiti huo walisema kwamba walikuwa wamechelewesha au walikwepa matibabu kwa kuhofia kutibiwa vibaya au walibadilisha madaktari mara kwa mara.

Soma pia:Wajerumani wenye asili ya Afrika walivyo na malengo ya juu 

"Takwimu zetu zinaonyesha kwamba uzoefu wa ubaguzi na ubaguzi wa rangi pia unahusishwa kwa uwazi sana na matatizo ya wasiwasi au dalili za huzuni," alisema mkurugenzi mwenza wa DeZIM Frank Kalter.

Mwanasoka Kingsley Ehizibue: 'Bila shaka ubaguzi wa rangi huniathiri'

Mkurugenzi wa DeZIM Naika Foroutan, ambaye anataka kuanzishwa kwa mfumo wa kudumu wa kufuatilia ubaguzi, alisema uzoefu wa kujirudia wa ubaguzi una madhara kwa afya na unahusishwa kwa karibu na upotevu wa imani katika taasisi za serikali, jambo ambalo anasema linaweza kutishia demokrasia.

Pendekezo lake kwa wanasiasa na jamii: Kubuni hatua za kuzuia ili kusaidia vyema zaidi wale walioathirika na mashirika ya kiraia "yanayofanya kazi kila siku kwa ajili ya jamii ya kidemokrasia, huru na yenye amani."

Rangi ya ngozi au jina la ukoo kamwe havipaswi kuwa sababu ya kuamua juu ya ubora wa huduma ya matibabu, nani anapata miadi ya daktari au anaweza kuanza matibabu, alionya Reem Alabali-Radovan, Kamishna wa Ushirikishwaji wa Serikali ya Shirikisho. Madaktari, wafanyikazi wa wauguzi na hospitali wanahitaji "mafunzo na dhana za kupinga ubaguzi wa rangi," alisema.Matakwa sawa na hayo yametolewa kuhusiana na wafanyakazi wa ofisi za umma.

Ubaguzi wa kijinsia na umri
Watu Weupe pia waliripoti kupitia ubaguzi. Kwa mujibu wa utafiti huo, wanawake walilalamika kuhusu mitazamo ya kijinsia, na wanaume kwa sababu ya ubaguzi wa ki umri.

Reem Alabali-Radovan Lagebericht "Rassismus in Deutschland"
Kamishna wa shirikisho anaeshughulikia ushirikishwaji wa wageni katika jamii ya Ujerumani, Reem Alabali-Radovan, anasema ngozi na jina la ukoo havipaswi kuwa msingi wa kutoa huduma kwa mtu.Picha: Christian Ditsch/epd-bild

Soma pia: Visa vya ubaguzi vimeongezeka Ujerumani

Utafiti huu utafuatiwa na nyingine. DW imefahamu kwamba, kufuatia vita vya Israel na Hamas, ripoti inayofuata itajikita juu ya chuki dhidi ya Wayahudi. Kituo cha ushirikishaji na uhamiaji cha Ujerumani, DeMIZ, kinachofadhiliwa na wizara ya mamo ya ndani, kimeomba kufanya utafiti huo.

"Ili kuweza kuchukua hatua makhsusi na zenye ufanisi dhidi ya ubaguzi, tunahitaji matokeo ya kisayansi zaidi na data za mara kwa mara, alisema waziri wa familia Lisa Paus, alisema baada ya kuulizwa na DW, .