1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tanzania yazindua kituo cha kutoa tahadhari ya majanga

Deo Kaji Makomba
14 Juni 2024

Kutokana na ukosefu wa mifumo madhubuti ya maonyo ya majanga, huko nchini Tanzania kumezinduliwa kituo cha ufuatiliaji mwenendo wa majanga na tahadhari ya mapema ambacho ni cha kwanza barani Afrika.

https://p.dw.com/p/4h3ki
Kituo cha kutoa tahadhari ya mapema ya kutokea majanga Tanzania
Tanzania yazindua kituo cha ufuatiliaji mwenendo wa majanga na tahadhari ya mapemaPicha: DeoKaji Makomba

Mabadiliko ya tabia nchi na maendeleo duni yanaelezwa kuzidisha hali ya hatari iliyopo na itafanya mifumo ya sasa ya tahadhari ya mapema na mifumo mingine ya kudhibiti hatari ya maafa kutokuwa na umuhimu.

Tanzania kama zilivyo nchi nyingine imeendelea kuchukua hatua mbalimbali za kujiandaa na kukabiliana na maafa kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa maendeleo wa ndani na nje ya nchi.

Katika kutekeleza hilo, Serikali ya Tanzania imeshiriki katika utekelezaji wa mradi wa uanzishaji wa Chumba cha Ufuatiliaji wa Majanga na tahadhari za Mapema ikiwa ni pamoja na kuandaliwa kwa jukwaa la kieletroniki lijulikanalo kama myDEWETRA.

Eneo la Katesh liliharibiwa na mafuruko
Zaidi ya watu 50 walikufa katika mafuruko yaliyolikumba eneo la Katesh kaskazini mwa Tanzania mwaka wa 2023Picha: Uncredited/AP Photo/picture alliance

Soma pia: Rais Samia aagiza hatua za haraka kusaidia wahanga wa mafuriko

Akizungumza katika uzinduzi wa kituo hicho katika eneo la Mtumba jijini Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Bunge na Uratibu, Jenista Mhagama amesema kuwa kituo hicho kitasaidia kutambua kwa mapema majanga ya asili yanayokuwa yakitokea na hivyo kuweza kuchua hatua za haraka ili kuzuia maafa makubwa.

Soma pia: Kimbunga Hidaya chaharibu miundombinu Tanzania

Udhibiti wa majanga mbalimbali yakiwemo ya asili unaelezwa kuwa ni Changamoto barani Afrika huku asilimia 40 tu ya watu barani humo ikiwemo nchi ya Tanzania, wakielezwa kupata mifumo ya hadhari ya mapema kutokana na hali ya juu ya hatari na ukosefu wa mifumo madhubuti ya maonyo ya hatari nyingi.

Athari za mafuriko na kimbunga kusini mwa Tanzania

Jane Alfred Kikunya ni mkurugenzi msaidizi wa kituo cha oparasheni na mawasiliano ya dharura kutoka katika ofisi ya Waziri mkuu anaelezea namna kituo hicho kitakavyokuwa kikifanya kazi.

Mradi wa uundaji wa jukwaa hili umeufanya kwa kushirikiana na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kupunguza Madhara ya Maafa katika Kanda ya Afrika kwa ufadhili wa Serikali ya Italia kupitia Shirika la Maendeleo la Italia na kutekelezwa na Taasisi ya CIMA Research Foundation ya Italia.