1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tanzania si chaka la wala rushwa - Rais Samia

11 Julai 2023

Rais Samia Suluhu Hassan wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amewaonya wala rushwa wa kimataifa watambuwe kwamba nchi yake si mahala salama kwao kujificha na kuendeleza vitendo vya kifisadi na utakatishaji fedha.

https://p.dw.com/p/4TkN9
Tansania Kamala Harris  Samia Suluhu Hassan
Picha: Ericky Boniphace/AP/picture alliance

Rais Samia aliyasema hayo katika kilele cha maadhimisho ya Siku ya Kupambana na Rushwa  Afrika yaliyofanyika jijini Arusha siku ya Jumanne (Julai 11) na kuhudhuriwa na viongozi wa taasisi za rushwa kutoka nchi mbalimbali za Afrika.

Akizungumza katika maadhimisho hayo, kiongozi huyo wa Tanzania alisema nchi yake si kichaka cha kuficha fedha za rushwa na wala si salama kwa  wala rushwa.

Soma zaidi: Rais wa Tanzania azindua mkutano wa mabunge wa SADC

"Nawashauri wanasiasa, viongozi wa serikali, ofisi ya Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai, na taasisi za kupambana na rushwa kwenda katika nchi zilizofanikiwa ili kujifunza kutoka kwao na kusaidia nchi katika mapambano dhidi ya rushwa," alisema Rais Samia huku akiwataka wadau wa mapambano hayo kutafakari na kubainisha changamoto na vikwazo na kila mmoja kutimiza wajibu wake katika mapambano hayo.

Mkataba wa Afrika wa Kupambana na Rushwa

Tansania Daressalam | State House | Samia Suluhu Hassan, Präsidentin & Gruppenfoto
Rais Samia Suluhu Hassan (katikati waliokaa) akiwa kwenye picha ya pamoja na viongozi wa serikali yake na vyama vya siasa.Picha: Ericky Boniphace/DW

Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (TAKUKURU), Kamishna wa Polisi Salum Hamduni alisema maadhimisho ya mwaka huu yanakwenda sambamba na maadhimisho ya miaka 20 ya utekelezaji wa Mkataba wa Afrika wa Kupambana na Rushwa uliowekewa azimio tarehe 3 Julai 2017.

Kinagaubaga: Je, uzalendo umepotea nchini Tanzania?

"Tanzania ilitia saini na kuridhia Mkataba wa Afrika wa Kupambana na Rushwa kama zilivyofanya nchi nyingine 55 za Afrika." Alisema Hamduni.

Katika maadhimisho hayo, Makamu Mwenyekiti wa Bodi ya Ushauri ya Kupambana na Rushwa Barani Afrika (AUABC), Pascoal Joaqium, alisema bodi yake ilipokea ripoti za mataifa 15 wanachama juu ya juhudi zao za kuzuia na kupambana na rushwa, ikiwemo Tanzania.

Imeandaliwa na Florence Majani/DW Dar es Salaam