1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroBangladesh

Watu karibu 100 wafa maandamano ya Bangladesh

Sylvia Mwehozi
5 Agosti 2024

Takriban watu 100 wameuawa na mamia ya wengine kujeruhiwa jana Jumapili wakati wimbi jipya la maandamano dhidi ya serikali likizidi kuenea kote nchini Bangladesh.

https://p.dw.com/p/4j6d6
Dhaka 2024 | Maandamano
Maandamano ya Bangladesh 2024Picha: Sazzad Hossain/DW

Waandamanaji wanamshinikiza waziri mkuu Sheikh Hasina ajiuzulu huku kiongozi huyo akiwashutumu waandamanaji kwa hujuma na kukata mawasiliano ya simu kwa nia ya kuzima machafuko.

Gazeti la kila siku la lugha ya Kibengali nchini humo, Prothom Alo, lilisema takriban watu 95, wakiwemo maafisa wa polisi 14, walikufa katika ghasia hizo. Kituo kingine cha habari cha Channel 24 kimeripoti vifo vya watu wasiopungua 85.

Jeshi limetangaza kuwa amri mpya ya kutotoka nje imeanza kutumika Jumapili jioni kwa muda usiojulikana, ikijumuisha katika mji mkuu wa Dhaka na makao makuu mengine ya tarafa na wilaya. Hapo awali serikali ilikuwa imeweka amri ya kutotoka nje isipokuwa baadhi ya maeneo ya Dhaka na kwingineko.

Maandamano |Bangladesh |Dhaka 2024
Maandamano ya Bangladesh Agosti 4Picha: Sazzad Hossain/DW

Waandamanaji wanamtaka Waziri Mkuu Hasina ajiuzulu kufuatia maandamano ya mwezi uliopita yaliyoanzishwa na wanafunzi wakitaka kusitishwa kwa mfumo wa ajira serikalini wanaodai ulikuwa na upendeleo. Maandamano hayo yalizidi kuwa ya ghasia na kusababisha vifo vya zaidi ya watu 200.Watu 8 wauawa katika maandamano ya kuipinga serikali nchini Bangladesh

Wakati vurugu hizo zikiendelea, Hasina alisema waandamanaji walioshiriki katika "hujuma" na uharibifu hawakuwa wanafunzi tena bali ni wahalifu, na kuongeza kuwa watu wanapaswa kuwashughulikia kwa mikono ya chuma.

Chama tawala cha Awami League kilisema shinikizo la kumtaka Hasina kujiuzulu, linaonyesha kuwa maandamano hayo tayari yametekwa na chama kikuu cha upinzani cha Bangladesh Nationalist Party na chama ambacho sasa kimepigwa marufuku cha Jamaat-e- Islami.Maelfu ya wabangladesh waadamana kudai haki za waliouawa

Serikali pia imetangaza mapumziko ya umma ya siku tatu kuanzia leo Jumatatu hadi Jumatano. Mahakama zitapaswa kufungwa kwa muda usiojulikana. Huduma ya mawasiliano ya simu huku mitandao ya kijamii ya Facebook na mingine ikiwa ni pamoja na WhatsApp, pia imezimwa.

Bangladesh | Maandamano
Waandamanaji wakipaza sauti zao wakati wa maandamano ya Bangladesh Picha: Mohammad Ponir Hossain/REUTERS

Takriban watu elfu 11,000 wamekamatwa katika wiki za hivi karibuni. Machafuko hayo pia yamesababisha kufungwa kwa shule na vyuo vikuu kote nchini.Bangladesh yakabiliwa na maandamano zaidi

Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Volker Turk amesema "ghasia za kutisha nchini Bangladesh lazima zikomeshwe," na kuelezea wasiwasi wake kuhusu vifo zaidi kabla ya maandamano makubwa huko Dhaka yaliyopangwa kufanyika Jumatatu. Aidha mkuu huyo ameitaka serikali nchini humo kuacha kuwalenga waandamanaji katika maandamano ya amani.

Siku ya Jumapili, wizara ya mambo ya nje ya India "iliwashauri" raia wake kutosafiri kwenda nchi jirani ya Bangladesh kufuatia ghasia hizo.