1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaMarekani

Marekani: Bunge laanzisha uchunguzi wa kumshtaki rais Biden

13 Septemba 2023

Spika wa Bunge la Marekani Kevin McCarthy amesema jana Jumanne kuwa ameanzisha uchunguzi utakaobaini iwapo rais Joe Biden anapaswa kushtakiwa na hatimaye kuondolewa madarakani.

https://p.dw.com/p/4WGUu
USA | Joe Biden und Kevin McCarthy
Picha: Jacquelyn Martin-Pool/Getty Images

McCarthy amesema uchunguzi wa awali uliofanywa mwaka huu na Bunge kwa familia ya Biden, umefichua kile alichokiita "utamaduni wa ufisadi" ambao anadai unahitaji uchunguzi wa kina. Spika huyo amesisitiza kuwepo madai ya matumizi mabaya ya madaraka na ufisadi.

Ikulu ya Marekani imezitaja juhudi hizo kuwa za mrengo mbaya wa kisiasa, huku Msemaji wa Ikulu hiyo ya White House Ian Sams akisisitiza kuwa  Wabunge wa Republican wamekuwa wakimchunguza Rais Biden kwa miezi 9, na hawajapata ushahidi wowote wa makosa hayo.

Baraza la wawakilishi la Marekani lina nguvu ya kumshitaki rais kwa wingi mdogo wa kura, lakini baraza la Seneti linahitaji wingi wa theluthi mbili kumuondoa rais madarakani, hatua ambayo sio rahisi kufanyika. Hadi sasa, hakuna rais wa Marekani aliyeondolewa madarakani kupitia mchakato huu wa Bunge.