1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Ripoti ya Umoja wa Mataifa kuhusu UKIMWI

18 Julai 2018

Kwa mujibu wa ripoti ya Umoja wa Mataifa, idadi ya watu wenye virusi vya ukimwi wanaopatiwa dawa imeongezeka zaidi. Kulingana na ripoti hiyo watu milioni 21.7 wanaogua maradhi hayo duniani kote wanatumia dawa hizo.

https://p.dw.com/p/31hkh
Ban Ki-moon und Charlize Theron auf der Pressekonferenz der International AIDS Conference 2016
Picha: picture-alliance/dpa

Shirika la Umoja wa Mataifa linalowasaida watu walioathirika na virusi vya ukimwi, UNAIDS limesema leo kuwa katika kila watu watano wenye virusi hivyo, watatu wanatumia dawa duniani kote. Kwa mujibu wa takwimu za shirika hilo watu milioni 36.9 walikuwa na virusi vya ukimwi hadi mwaka uliopita duniani kote. Na kati ya hao milioni 15.2 hawakuwa wanapata dawa walizohitaji.

Licha ya kupatikana mafanikio katika kuzuia maambukizi mapya na vifo, shirika la UNAIDS linasikitika juu ya kuongezeka idadi ya watu walioathirika. Takriban watu milioni 80 waliambukizwa virusi vya ukimwi na milioni 35.4 wamekufa tangu kuripotiwa kwa mikasa ya kwanza mnamo miaka ya 80. Mkurugenzi mtendaji wa shirika la UNAIDS Michel Sidibe amesema awali ilikuwa ni idadi ya watu wachache tu ndio waliopokea matibabu lakini kwa sasa idadi hiyo imeongezeka kwa karibu watu milioni 22 wanaopata matibabu.

Mkurugenzi mtendaji wa UNAIDS Michel Sidibe
Mkurugenzi mtendaji wa UNAIDS Michel SidibePicha: picture alliance/ZUMAPRESS

Shirika hilo la Umoja wa Mataifa linalopambana na maradhi ya ukimwi pia limetahadhrisha juu ya hatari ya kukwama na kurudi nyuma kwa juhudi za kupambana na maradhi hayo ikiwa fedha zaidi hazitapatikana na ikiwa juhudi hizo zitapuuzwa duniani.

Shirika hilo limesema pana hatari ya kurudi nyuma kwa hatua iliyofikiwa hadi sasa katika harakati ya kupambana na maradhi ya ukimwi .Mkurugenzi wa shirika hilo Michel Sidibe amesema asasi yake imepungukiwa dola bilioni 7 zinazohitajika ili kuweza kuendeleza mafanikio yaliyokwishapatikana hadi sasa na  ili kuweza kuyafikia malengo  ya  shirika mnamo mwaka 2020.Bwana Sidibe amesema bila ya fedha  hizo kupatikana ,itakuwapo hatari kubwa ya kurudi upya kwa idadi kubwa ya maambukizi. Mnamo mwaka uliopita dola bilioni 20 zilitengwa kwa ajili ya nchi zenye vipato vya chini na nchi zenye vipato vya kati. Nchi hizo zilichangia asimilia 56 kutokana na bajeti zao. Hata hivyo Marekani ambayo hadi sasa imekuwa mfadhili mkubwa kabisa, imetishia kukata misaada chini ya utawala wa rais Donald Trump.

Soweto: Michoro ukutani inaonesha kwamba UKIMWI unaua
Soweto: Michoro ukutani inaonesha kwamba UKIMWI unauaPicha: picture-alliance/dpa

Lengo la Umoja wa Mataifa ni kuwawezesha asilimia 90 ya watu wenye virusi vya ukimwi,kujua hali zao hadi mwaka wa 2020. Takriban asilimia 90 miongoni mwao wanapaswa kupatiwa dawa za kudumaza makali ya virusi vya ukimwi, ARV na dawa za kuzuia kabisa kulipuka kwa ugonjwa huo mwilini.

Licha ya kufanyika juhudi kubwa za utafiti katika kipindi cha miaka zaidi ya 30 mpaka sasa haijapatikana dawa ya kutibu maradhi ya UKIMWI. Hata hivyo katika eneo la mashariki na kusini mwa Afrika idadi ya vifo imepungua kwa asilimia 42 kati ya mwaka 2010 na 2017. Asilimia 53 ya watu wenye virusi vya ukimwi duniani wanaishi katika sehemu hiyo ya Afrika.

Mwandishi:Zainab Aziz/AFPE

Mhariri: Iddi Ssessanga