1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaNiger

Ufaransa kuwaondoa wanajeshi wake walioko Niger

25 Septemba 2023

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amesema ushirikiano wa kijeshi na Niger utafikia mwisho na wanajeshi wake waliokuwa nchini humo watarejeshwa nyumbani ifikapo mwishoni mwa mwaka.

https://p.dw.com/p/4Wkwi
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ameahidi kuyaondoa majeshi ya Ufaransa nchini Niger kufuatia upinzani mkali kutoka nchini humo. Hapa rais Macron alikuwa katika mkutano wa G20, mjini New Delhi, Septemba 10, 2023
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ameahidi kuyaondoa majeshi ya Ufaransa nchini Niger kufuatia upinzani mkali kutoka nchini humo. Hapa rais Macron alikuwa katika mkutano wa G20, mjini New Delhi, Septemba 10, 2023Picha: Amit Dave/REUTERS

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron ametangaza jana Jumapili kwamba Ufaransa itawaondoa wanajeshi wake nchini Niger pamoja na kumrejesha nyumbani balozi wake baada ya mapinduzi ya kijeshi yaliyomuondoa madarakani rais Mohamed Bazoum.

Tangazo hilo, ni pigo kubwa dhidi ya sera za Ufaransa barani Afrika, baada ya wanajeshi wa taifa hilo pia kuondoka taifa jirani la Mali na Burkina Faso katika miaka ya karibuni baada ya kukumbwa na mapinduzi.

Ufaransa iliwabakiza wanajeshi wake 1,500 nchini Niger tangu mapinduzi ya Julai na mara kadhaa imekaidi agizo la utawala mpya wa kijeshi la kumuondoa balozi wake, kwa kuwa Ufaransa haiutambui utawala huo.  

Soma pia: Raia waandamana Niger kutaka Ufaransa iondoe wanajeshi wake 

Taifa hilo lilipeleka maelfu ya wanajeshi kwenye ukanda wa Sahel baada ya wakuu wa mataifa hayo kuiomba kusaidia harakati zao za kupambana na ugaidi.

Utawala wa kijeshi wa Niger wafurahishwa na tangazo la kuondolewa wanajeshi wa Ufaransa

Watawala wa kijeshi wa Niger jana Jumapili walikaribisha tangazo hilo la Ufaransa ikilitaja kama "hatua mpya kuelekea uhuru".

Wanajeshi wa Ufaransa wakiwa kwenye moja ya operesheni zake za kupambana na uasi katika ukanda wa Sahel. Hata hivyo Ufaransa imeendelea kuwaondoa wanajeshi hao, baada ya mataifa ya ukanda huo kushinikiza waondolewe, ikiwa ni pamoja na Niger
Wanajeshi wa Ufaransa wakiwa kwenye moja ya operesheni zake za kupambana na uasi katika ukanda wa Sahel. Hata hivyo Ufaransa imeendelea kuwaondoa wanajeshi hao, baada ya mataifa ya ukanda huo kushinikiza waondolewe, ikiwa ni pamoja na Niger Picha: Frederic Petry/Hans Lucas/picture alliance

Utawala huo ulitoa kauli hiyo saa chache baada ya Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron kutangaza pia kwamba hivi karibuni Paris itamuondoa balozi wake kutoka Niger, katika miezi ijayo.

"Jumapili hii, tunasherehekea hatua mpya kuelekea uhuru wa Niger," ilisema taarifa ya watawala wa kijeshi wa nchi hiyo, walionyakua mamlaka mwishoni mwa Julai kwa kumpindua rais Mohamed Bazoum mnamo Julai 26.

"Wanajeshi wa Ufaransa na balozi wa Ufaransa wataondoka katika ardhi ya Niger ifikapo mwisho wa mwaka," imeongeza taarifa hiyo iliyosomwa kwenye televisheni ya taifa: "Huu ni wakati wa kihistoria, ambao unazungumzia dhamira na mapenzi ya watu wa Niger."

Soma Pia: Mkuu wa Jumuiya ya ECOWAS apendekeza kipindi cha miezi 9 nchini Niger 

Mapema Jumapili, kabla ya tangazo la Macron, chombo kinachosimamia usalama wa anga barani Afrika (ASECNA), kilitangaza kuwa watawala wa kijeshi wa Niger wamepiga marufuku "ndege za Ufaransa" kuruka juu ya anga ya nchi hiyo.

Mvutano umeongezeka katika wiki za hivi karibuni kati ya Ufaransa na Niger, ambayo nikoloni la zamani la Ufaransa. 

Ali Sekou Ramadan, msaidizi wa Rais aliyeondolewa madarakani wa Niger Mohamed Bazoum, aliiambia shirika la habari la Associated Press kwamba Bazoum alimuomba Macron kumwondoa balozi wa Ufaransa, Sylvain Itte, "ili kupunguza mvutano."