1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Rais Biden alazimika kusitisha kampeni zake

18 Julai 2024

Rais wa Marekani Joe Biden amesitisha kampeni zake baada ya kugundulika na virusi vya UVIKO-19 muda mfupi baada ya kukubali kwamba hatowania urais ikiwa madaktari watathibitisha kuwa hali yake ya kiafya sio imara.

https://p.dw.com/p/4iSa0
Uchaguzi wa Marekani 2024 Joe Biden baada ya kugundulika na virusi vya UVIKO.
Rais Joe Biden akipanda ngazi za Air Force One kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Harry Reid huko Las Vegas, Baada ya kugundulika na virusi vya UVIKOPicha: Susan Walsh/AP Photo/picture alliance

Kwa upande mwingine mkutano mkuu wa chama cha Republican uliendelea hapo jana ambapo mteule wa nafasi ya mgombea mwenza wa Trump, JD Vance alipanda jukwaani kujitambulisha na kumsifu Donald Trump kwa namna alivyoshugulikia jaribio la kumuua.

Biden mwenye umri wa miaka 81 aliwaonyesha waandishi wa habari dole gumba na kusema "najisikia vizuri" alipositisha ziara yake Las Vegas na kuelekea nyumbani kwake Delaware ili kujitenga, jambo ambalo litamtoa nje ya kampeni ya siku kadhaa.

Maambukizi hayo yanajiri katika wakati mgumu kwa kampeni ya Biden, huku rais huyo akitaka kuonyesha kuwa yuko tayari kuendelea na kibarua baada ya kufanya vibaya katika mjadala dhidi ya mpinzani wake Donald Trump na kuzua wasiwasi juu ya afya yake na wito kutoka kwa baadhi ya Demokrats kumtaka ajitoe kwenye kinyanganyiro hicho.

Kwa mujibu wa msemaji wake, Karine Jean-Pierre,  Biden aliyekuwa tayari amepata chanjo ya UVIKO na kadhalika ile ya kuongezewa nguvu na sasa anatumia dawa na "anaendelea kutekeleza majukumu kamili ya ofisi akiwa karantini." 

Marekani| Karine Jean-Pierre
Msemaji wa Ikulu ya White House Karine Jean-Pierre akizungumza na waandishi wa habari.Picha: Mandel Ngan/AFP

Daktari wa Ikulu ya Marekani Kevin O'Connor alisema Biden alilalamika kusumbuliwa na mafua, kikohozi na dalili za homa na mara baada ya kuhudhuria hafla ya kampeni alipimwa na kugundulika na virusi hivyo.

Soma pia: Biden: Niko sawa kiafya hivyo msiwe na hofu

Haya yanajiri wakati  wasiwasi ukizidi kuongeza juu ya afya ya rais mkongwe zaidi wa Marekani katika historia ya Amerika. Alipoulizwa nini kinaweza kumfanya afikirie upya nia yake ya kuwania urais, Biden alikiambia chombo cha habari cha Black BET katika mahojiano yaliyorekodiwa Jumanne huko Las Vegas.

"Ikiwa nitakuwa na aina flani ya ugonjwa ambao utajitokeza, au mtu, au daktari aje kuniambia kuwa una tatizo hili au lile."

"Nilifanya makosa makubwa wakati wa mdahalo na kumbuka kwamba wakati nilipowania urais mara ya kwanza nilipasa kuwa rais wa mpito. Nilidhani nitaweza kuondokana na kumpisha mtu mwengine."

"Sikutarajia kwamba mambo yangegawanyika. Kiukweli nafikiri kitu ambacho umri unazidisha ni busara kidogo."

Soma pia: Biden asema hang'oki licha ya makosa ya aibu

J.D Vance ajitambulisha rasmi

Marekani | Donald Trump und JD Vance
Donald Trump akiwa na mgombea mwenza wa J.D Vance wakati wa kampeni zao Marekani.Picha: Gaelen Morse/REUTERS | Andrew Kelly/REUTERS

Huku haya yakijiri mkutano mkuu wa chama cha Republican umeendelea hapo jana ambapo mteule wa nafasi ya mgombea mwenza wa Trump, J.D Vance alipanda jukwaani kujitambulisha na kumsifu Donald Trump kwa namna alivyoshuguliki jaribio la mauaji dhidi yake.

Katika hotuba yake ya kwanza rasmi tangu alipochaguliwa kuwa mgombea mwenza wa Trumpsiku ya Jumatatu, Vance alitoa maelezo madhubuti ya kukua katika umaskini, bila baba nyumbani na mama mraibu wa dawa za kulevya.

Ulikuwa utambulisho rasmi wake wa kwanza kwa watu wengi na kampeni ya Trump inategemea hotuba hiyo kuwashawishi  wapiga kura wenye msimamo mkali katika majimbo yenye ufunguo wa kushinda uchaguzi wa marudio wa Novemba dhidi ya Rais Joe Biden.