1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaIndonesia

Papa Francis awasili Indonesia

3 Septemba 2024

Kiongozi wa kanisa Katoliki duniani Papa Francis amewasili nchini Indonesia kuanza ziara ya mataifa manne ya Asia-Pasifiki ambayo itakuwa ndefu na ya mbali zaidi ya kiongozi huyo wa kidini mwenye umri wa miaka 87.

https://p.dw.com/p/4kDMP
Indonesia | Ziara ya Papa Francis Indonesia Jakarta
Papa Francis akipokea shada la maua, lililotolewa na watoto wawili waliovalia kitamaduni.Picha: Agus Suparto/Indonesia Papal Visit Committee/Anadolu/picture alliance

Ziara hii ni ya 45 ya kiongozi huyo wa kanisa katoliki nje ya nchi,ambayo inalenga kuhimiza amani na mshikamano kati ya dini mbalimbali.

Kwa kuzingatia umri na hali ya afya ya Papa Francis, ambaye sasa mara nyingi hutumia kiti cha magurudumu, muda wa mapumziko baada ya safari zake za kigeni umekuwa mrefu zaidi.

Papa aliwapungia mkono watu wengi waliojitokeza kumlaki kando ya barabra wakati wa msafara wake.

Akibubujikwa na machozi Maria Celine, alielezea furaha yake baada ya kumuona  kiongozi huyo wa kidini.

"Ninajivunia na kuguswa sana kwa sababu tuko katika nchi ya Kiislamu na bado tunatembelewa na papa, kiongozi mkuu wa Kikatoliki."

Uwiano wa kidini

Katika ziara hiyo ya siku 12 Papa Francis atazitembelea pia Papua New Guinea,Timor ya Mashariki na Singapore.

Papa Francis aanza ziara Indonesia
Kiongozi wa kanisa katoliki aanza ziara yake ya mataifa manne ya asia-pasifiki nchini Indonesia.Picha: VATICAN MEDIA/AFP

Papa atapumzika mjini Jakarta, kisha kukutana na Rais Joko Widodo kesho Jumatano katika sehemu kuu ya kwanza ya ziara yake katika nchi hiyo yenye Waislamu wengi zaidi duniani.

Indonesia inahesabika kuwa nchi yenye idadi kubwa ya waislamu duniani, wanaofikia milioni  240 wakati Timor mashariki ndiyo yenye idadi kubwa ya wakristo katika nchi ambazo Papa Francis atazitembelea.

Mkutano na viongozi wa kidini

Indonesia | Imamu Mkuu wa Msikiti wa Istiqlal Nasaruddin Umar
Imamu Mkuu wa Msikiti wa Istiqlal Nasaruddin Umar alisisitiza kwamba kuwasili kwa Papa Francis nchini Indonesia ni aina ya uvumilivu kati ya jumuiya za kidini.Picha: Levie Wardana/DW

Siku ya Alhamisi, Papa Francis atakutana na wawakilishi wa dini au madhehebu sita yanayotambulika rasmi nchini Indonesia katika Msikiti mkubwa zaidi Kusini-mashariki mwa Asia wa Istiqlal, ishara ya uwiano wa pamoja kidini.

Kulingana na maaskofu wa Indonesia, katika Msikiti wa Istiqlal, Papa Francis anatarajiwa kutia saini tamko la pamoja na imamu mkuu, ambalo litazingatia kupinga udhalilishaji, haswa kutokana na kuenea kwa ghasia na migogoro, pamoja na uharibifu wa mazingira.

Kisha ataongoza misa na kutoa mahubiri katika uwanja wa taifa wa kandanda wenye uwezo wa kuchukua watu 80,000.

Lakini licha ya Indonesia kutambuwa rasmi imani tofauti, kuna wasiwasi kuhusu kuongezeka kwa ubaguzi, ikiwa ni pamoja na dhidi ya Wakristo, huku Wakatoliki wa eneo hilo wakitumai papa atazungumza changamoto hiyo.

Ziara hii ya Papa Francis nchini Indonesia ni ya tatu kuwahi kufanywa na papa na ya kwanza tangu John Paul II mwaka 1989. Hapo awali ilipangwa kwa 2020 lakini iliahirishwa kutokana na janga la UVIKO.