1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Papa Francis ahimiza amani katika hotuba yake ya Pasaka

Zainab Aziz Mhariri: Bakari Ubena
17 Aprili 2022

Kiongozi wa kanisa Katoliki duniani Papa Francis, ameongoza misa ya Jumapili ya Pasaka katika uwanja wa kanisa la Mtakatifu Peter mjini Vatican. Papa Francis ametoa wito wa kuzingatiwa amani.

https://p.dw.com/p/4A2pj
Vatikanstadt | Ostermesse Papst Franziskus - "Urbi et Orbi"
Picha: TIZIANA FABI/AFP/Getty Images

Papa Francis amewataka viongozi kusikia vilio vya watu wanaotaka amani nchini Ukraine. Amesema amesikitishwa kuwa Pasaka ya mwaka huu ni Pasaka iliyogubikwa na vita.

Papa Francis akiongoza ibada ya "Urbi et Orbi" katika kanisa la Mtakatifu Peter mjini Vatican.
Papa Francis akiongoza ibada ya "Urbi et Orbi" katika kanisa la Mtakatifu Peter mjini Vatican.Picha: TIZIANA FABI/AFP/Getty Images

Papa Francis ameilaumu tabia ya kutunishiana misuli huku watu wakiwa wanateseka nchini Ukraine lakini bila ya kumlaumu waziwazi Rais wa Urusi Vladimir Putin kwa uamuzi wake wa kuanzisha uvamizi na mashambulio dhidi ya Ukraine mnamo Februari 24.

Akizungumza na takriban watu 50,000 waliohudhuria ibada hiyo ya Jumapili ya Pasaka katika kanisa la mtakatifu Peter, katika misa anayoiongoza mara mbili kwa mwaka ya "Urbi et Orbi" kwa ajili ya jiji la Vatican na ulimwengu kwa jumla, Papa Francis amesema Ukraine inakabiliwa na mtihani mkubwa sana wa kukumbwa na ghasia na uharibifu kutokana na vita vya kikatili visivyostahili kuwepo.

Papa Francis mwenye umri wa miaka 85 kwenye sehemu kubwa ya hotuba yake, amezungumza juu ya migogoro ya dunia, pamoja na mgogoro wa sasa wa nchini Ukraine.

Papa Francis akipita mbele ya makadinali na viongozi wa Kanisa Katoliki wakati wa mkesha wa siku ya Pasaka.
Papa Francis akipita mbele ya makadinali na viongozi wa Kanisa Katoliki wakati wa mkesha wa siku ya Pasaka.Picha: Tiziana Fabi/AFP

Papa Francis ameeleza kwamba mzozo huu wa barani Ulaya uwafanye watu wawe na wasiwasi zaidi kuhusu nchi zingine zinazokabiliwa na migogoro, mateso na huzuni, hali ambazo zinaathiri maeneo mengi ulimwenguni. Miongoni mwa migogoro aliyotaja ni ile ya Mashariki ya Kati na amehimiza amani na upatanisho kwa watu wa Lebanon, Syria na Iraq. Pia ameyazugnumzia mataifa ya Libya na Yemen ambayo yanakabiliwa na migogoro inayoonekana kusahaulika na wote.

Vile vile Papa Francis katika siku ya Jumapili ya Pasaka ametoa wito wa kufunguliwa njia kwa watu kuyafikia maeneo matakatifu katika mji wa Jerusalem wakati ambapo ghasia zinaendelea kati ya Waisraeli na Wapalestina katika Jiji hilo Takatifu.

Mji mtakatifu wa Jerusalem
Mji mtakatifu wa JerusalemPicha: Ilan Rosenberg/REUTERS

Amesema anaomba amani iwepo katika Mashariki ya Kati, iliyogubikwa na mizozo na migawanyiko kwa miaka mingi. Hususan katika siku hii tukufu, Papa Francis amemtaka kila mtu aombe amani katika mji wa Jerusalem kwa wote Wakristo, Wayahudi na Waislamu wanaokaa katika jiji takatifu, pamoja na mahujaji na wakati huo huo amesisitiza umuhimu kwa jamii kukaa katika udugu na kufurahia nafasi ya kufika bila masharti yoyote mahala patakatifu kwa kuheshimianana kuzingatia haki za kila mmoja.

Vyanzo:AP/AFP/DPA