1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

NCHI ZA G20 KUKUTANA BERLIN

AHMED M SALEH19 Novemba 2004

Miaka mitano iliyopita, mjini Berlin liliundwa kundi la G20, yaani mwungano kati ya kundi la nchi saba muhimu za viwanda G7 na nchi muhimu zenye kipato wastani. Mwungano huo uliundwa kama jukwaa lisilo rasmi kwa Mawaziri wa Mambo ya Fedha na Wakurugenzi wa Mebenki Makuu kuzungumzia migogoro ya kifedha katika nchi zenye kipato wastani mnamo miaka ya 90. Mada kuu hii leo miongoni mwa nchi za G20 ni utulivu wa mifumo ya fedha, wakati mmoja zikifanywa juhudi za kuimarishwa mifumo ya ustawi wa kudumu wa kiuchumi. Mwaka huu Ujerumani imeanza kuwa Mwenye Kiti wa Kundi la G20, na mwishoni mwa wiki hii mjini Berlin utafanyika mkutano wa kila mwaka wa Mawaziri wa Mambo ya Fedha wa kundi hilo.

https://p.dw.com/p/CHi3

Japokuwa kwa hivi sasa ni bado ndoto, lakini kwa kipindi kirefu kijacho unazingatiwa uwezekano wa kundi la G20 kuchukua nafasi ya kundi la G7. Inajulikana kuwa wanachama wa kundi la G7 ni nchi za viwanda, Ujerumani, Ufaransa, Uitalia, Japan, Kanada, Uingereza na Marekani. Nchi hizi hutafuta muwafaka kuhusu matatizo moto moto yanayoibuka katika uchumi wa kimataifa kulingana na maslahi yao wenyewe ya kiuchumi. Upande wa pili kundi la G20 hujaribu kuendelezamaslahi kati ya nchi za viwanda na nchi zenye vipato wastani. Na japokuwa katika mikutano yao kundi hilo halifikii muwafaka katika umbo la kusainiwa mikataba, muwafaka unaofikiwa huwa zaidi kutangazwa shabaha zao za kisiasa zenye makusudi ya kushawishi siasa ya kiuchumi ya mataifa yao pamoja na kutekeleza mapatano yaliyofikiwa katika mashirika ya Fuko la Kimataifa la Fedha na Benki Kuu ya Dunia.

Wakati huo huo kundi hili lina niya ya kutunga mikakati ya pamoja ya kimataifa pamoja na kupendekeza harakati za kuimarisha maendeleo yao kupitia hatua za kupigiwa mfano. Hiyo ni shabaha ya hali ya juu japokuwa kundi hilo la nchi za G20 linadhibiti asili miya 90 ya pato ghafi la kimataifa, robo tatu ya biashara za kimataifa zikiwa zinawakilisha thuluthi mbili ya umma wa dunia. Tamngu kundi hilo la G20 liundwe mjini Berlin mwaka 1999, yamefanyika mabadiliko katika mizano ya nguvu za wanachama wake. Kwa mfano tayari leo uchumi wa baadhi ya nchi zenye vipato wastani, kama vile Uchina, unashawishi pakubwa ustawi wa nchi za G7. Kwa hivyo hii leo mjadala kuhusu maendelezo ya ustawi wa kimataifa wa uchumi hauwezekani bila ya kuingizwa nchi zenye vipato wastani vya kiuchumi kama vile Uchina, India, Brazil, na Afrika ya Kusini. Ulimwengu unazidi kujongelena na kutegemeana kiuchumi pamoja na kukuwa kiwango cha nchi zenye dhamana maalumu katika ustawi wa uchumi wa kimataifa.

Mjini Berlin mada kuu kabisa itahusika na ustawi wa uchumi wa kimataifa, hasa kufuatana na kule kupanda pakubwa bei ya mafuta. Hapa litawekwa mbele swali kwa njia gani inaweza kupatikana mizani baina ya viwango vya uzalishaji wa mafuta na mahitaji ya mafuta katika masoko ya kimataifa. Mada nyingine muhimu itahusika na kule kupanda na kushuka thamani ya sarafu ya Ulaya, EURO. Waziri wa Mambo ya Fedha wa Ujrumani Hans Eichel amekwisha sema kuwa swali hilo litazungumzwa kisiri, japokuwa alisisitiza kuwa anatumaini kuwa itaweza kuwiyanishwa misimamo kati yaa Japan, Marekani na Umoja wa Ulaya. Mada nyingine ya maana itahusika ni mifumo ya kifedha, hasa katika swali la kuwekwa katika mebenki rasmi fedha zinazochumwa kutoka biashara ya haramu pamoja na swali la ugaidi. Mada hiyo si mpya kabisa, kwani tayari mwishoni mwa 2001 zilitunga mpango wa utendaji katika kupigana na miundo ya kugharimia ugaidi wa kimataifa. Mpango huo wa utendaji unaingiza mambo kama kufunga akaunti za benki za makundi yanayoshutumiwa kuwa ya kigaidi, pamoja na kutangaza majina ya makundi yanayohusishwa na ugaidi. Kwanza wajunbe wa mkutano watakabidhiwa ripoti kuhusu maendeleo yaliyopatikana katika kampeni hiyo. Na hatimaye kuingizwa pia mada kuhusu mikakati ya kupigana na wizi wa kodi. Benki Kuu ya Dunia imethibitisha namna nchi zenye ustawi wastani wa kiuchumi pamoja na nchi zinazoendelea zilivyoumizwa na mitindi hiyo ya kuongezeka wizi wa kodi.