1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaIsrael

Mashambulizi ya Hamas dhidi ya Israel yalaaniwa

9 Oktoba 2023

Nchi nyingi wanachama wa Baraza la Usalama la UN zimelaani mashambulizi ya Hamas ya Jumamosi dhidi ya Israel, lakini Marekani na Israel zimekosoa kukosekana kwa kauli moja kutoka kikao cha dharura cha baraza hilo

https://p.dw.com/p/4XH4L

Waisraeli zaidi ya 700 waliuawa katika mashambulizi hayo ya Hamas, wakiwamo zaidi ya 260 waliouawa katika tamasha la muziki. Wapalestina wasiopungua 400 pia wamepoteza maisha katika hujuma za Israel za kulipiza kisasi katika Ukanda wa Gaza.

Soma pia:Baada ya shambulio la Hamas, Netanyahu asema Israel iko vitani

Wanadiplomasia wamearifu katika kikao cha Baraza la Usalama, baadhi ya mataifa yakiongozwa na Urusi yalitaka mkutano huo uangazie masuala mapana zaidi badala ya kujikita juu ya Hamas.

Mataifa kadhaa yatangaza kusimama na Israel

Wizara ya ulinzi ya Marekani imesema inapeleka manowari yake ya kubebea ndege za kivita mashariki mwa bahari ya Mediterania, huku waziri wa ulinzi wa Marekani Llyod Austin akithibitisha kuwa nchi yake itaipatia Israel msaada zaidi wa silaha, na kuimarisha uwepo wa kijeshi wa Marekani katika Ukanda wa Mashariki ya Kati.

Soma pia:Mashirika makubwa ya ndege yamefuta safari zao kuelekea katika mji mkuu wa Israel, Tel Aviv

Hali kadhalika Kansela wa Ujerumani Olaf Scholz amezungumza kwa njia ya simu na waziri mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, na kumhakikishia kuwa Ujerumani inasimama bega kwa bega na Israel.