1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MichezoUganda

Mwanariadha wa Uganda afariki baada ya mpenzi kumchoma moto

5 Septemba 2024

Madaktari na maafisa wa riadha wamesema mwanariadha wa Uganda Rebecca Cheptegei, aliyeshiriki katika michezo ya Olimpiki nchini Ufaransa amefariki nchini Kenya, Alhamisi, siku nne baada ya kuchomwa moto na mpenzi wake.

https://p.dw.com/p/4kIiR
Rebecca Cheptegei ameaga dunia
Rebecca Cheptegei, aliyeshiriki katika michezo ya Olimpiki nchini Ufaransa amefarikiPicha: Chai v.d. Laage/IMAGO

Rais wa Kamati ya Olimpiki ya Uganda, Donald Rukare, amesema kwenye mtandao wa X kwamba tukio hilo la mwanariadha Cheptegei kuuliwa na mpenzi wake ni la unyanyasaji wa kijinsia katika nchi hiyo ya Afrika Mashariki,  huku wanaharakati wakitahadharisha kuhusu janga la mauaji ya wanawake.

Kulingana na polisi ya Kenya, mwanamume anayetambuliwa kama mpenzi wa Cheptegei anayeitwa Dickson Ndiema Marangach, alimmwagia petroli na kumchoma msichana huyo siku ya Jumapili nyumbani kwake Endebess katika kaunti ya Trans-Nzoia, magharibi mwa Kenya.

Mkasa huo umetokea wiki chache tu baada ya Cheptegei, mwenye umri wa miaka 33, kushiriki mbio za marathon katika Michezo ya Olimpiki ya mjini Paris, ambako alishika nafasi ya 44.