1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaAsia

Mwaka wa msukosuko, mustakabaili wa mashaka kwa Afrghanistan

Hawa Bihoga
28 Desemba 2021

Baada ya Taliban kuchukua madaraka kwa namna ya kustajabisha nchini Afghanistan mwaka huu 2021, taifa hilo linakabiliwa na changamoto kadhaa, huku jumuiya ya kimataifa ikihofia kurejea tena kwa makundi ya itikadi kali.

https://p.dw.com/p/44vtc
Lokale Wirtschaft und Handel in Afghanistan
Picha: Mohd Rasfan/AFP/Getty Images

Kurudi madarakani kwa namna ya kustajabisha kwa kundi hilo lililokuwa la waasi kuliibua  mshtuko kwa Waafganistan na hata miongoni mwa Waislamu wenye msimamo mkali.

Changamoto kubwa kwa Taliban inayosubiriwa na wengi ni kuweza kubadilika kutoka  kikosi cha waasi na kuwa chombo cha utawala ambacho kinaweza kutawala taifa ambalo linashuhudia mgawanyiko mkubwa huku likakabiliwa na mahitaji mengi.

Kwa mataifa ya magharibi kama Marekani na washirika wake jumuiya ya kujihami NATO,  wasiwasi mkubwa ni wa namna mbili kutokana na Taliban kuchukua dola.

Soma pia: Taliban yaiandikia Marekani barua ya wazi kuihimza kuondoa vikwazo

Kwanza makundi ya kigaidi kama vile Al-Qaeda yatapata tena mahali salama kujiimarisha na kuendeleza shughuli zao, pili, hali itazidi kuwa mbaya na kusababisha makumi kwa maelfu ya Waafghanistan kukimbilia nje ya nchi wakihofia usalama wao.

Lokale Wirtschaft und Handel in Afghanistan
Watu wakifanya biashara mjini Kabul, Desemba 26, 2021.Picha: Mohd Rasfan/AFP/Getty Images

Upande wa  Waafghanistan wa kawaida  kwao chakula, malazi na ajira ni kipaumbele, huku wanawake hasa wakibeba mzigo mkubwa wa sera kandamizi za kijamii za Taliban.

Kate Clark aliandika katika ripoti maalum ya Mtandao wa Wachambuzi wa Afghanistan, AAN, akisema matokeo ya unyakuzi huo yalikuwa mabaya na ya ghafla, hawakuwa na mipango ya jinsi watakavyoendesha taifa la Afghanistan bila msaada, bali kushinikiza ushindi wa kijeshi.

Upinzani, waliwatoza kodi watu waliokuwa chini ya udhibiti wao ipasavyo, lakini waliweza kuacha huduma za umma  kwa serikali, mashirika yasio ya kiraia  na hatimaye wafadhili, Iliongeza taarifa ya Clark.

Soma pia: Je uvamizi wa Marekani Afghanistan uliibadilisha taifa hilo?

Kuporomoka kwa mifumo ya usimamizi

Moja ya changamoto kubwa ambayo inaikabilia Taliban kwa sasa ni kuporomoka kwa kiwango kikubwa kwa mifumo ya utawala.

Zaidi ya Waafghanistan 120,000 walihamishwa katika siku za mwisho za machafuko ya kujiondoa kwa Marekani, wengi kati yao walifanya kazi na mataifa ya kigeni katika kusimamia utawala na uchumi unaotegemea misaada.

Watumishi wengi wa umma walikuwa hawajalipwa kwa miezi kadhaa kabla ya Taliban kutwaa mamlaka, na wana motisha ndogo ya kurejea kazini bila kujua ni lini watapata mshahara.

Afghanistan Kabul | Protest für Freigabe der eingefrorenen Geldmittel
Watu wakishika bango lenye maneno yasemayo 'Tuacheni tule' kabla ya kuandamana mjini Kabul Desemba 21, 2021, wakati taifa hilo likipambana na mzozo mkubwa wa kiuchumi.Picha: Mohd Rasfan/AFP/Getty Images

Hazrullah ni mwanateknolojia wa ngazi ya kati katika wizara ya mambo ya nje amenukuliwa akisema, wanakwenda kazini lakini hakuna la kufanya, awali alikuwa akishughulikia mikataba ya kibiashara na mataifa jirani lakini kwa sasa hakuna maelekezo ya namna ya kuendelea na kazi na hakuna anaejua chochote.

Soma pia: Marekani yaanza kuondosha wanajeshi Afghanistan

Kwa watoa misaada ya kiutu bado kwao ni changamoto kubwa kwani takriban  watu milioni 23, au asilimia 55 ya watu, wanakabiliwa na uhitaji wa dharura wa chakula msimu huu wa baridi, imesema  Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu, OCHA katika taarifa yake.

Wafadhili wana wasiwasi kuhusu kusaidia utawala wa itikadi kali, wakati Taliban wanaamini ushindi wao haupaswi kuathiriwa kwa kuruhusu wanawake kufanya kazi.

Hivi karibuni baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio lililopendekezwa na Marekani la kusaidia misaada ya kibinadamu kuwafikia Waafghanistan waliokata tamaa huku likitafuta kuzuia fedha kutoka mikononi mwa Taliban.

Lakini Taliban imesisitiza haiwezi kuamriwa na mataifa na mashirika ya kigeni na  lazima kuwe na udhibiti wa ufadhili na misaada  jambo ambalo bado haliwapendezi wafadhili wengi.

Tayari baadhi ya mashirika ya kutoa misaada ya kibinaadam yameweza kusambaza vifaa muhimu kwa wahitaji

Chanzo: AFP