1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
SiasaUturuki

Ankara: Mlipuko wa bomu karibu na Bunge la Uturuki

1 Oktoba 2023

Wizara ya Mambo ya Ndani ya Uturuki imesema magaidi wawili wameshambulia kwa bomu mbele ya majengo ya wizara hiyo iliyo karibu na Bunge katika mji mkuu, Ankara.

https://p.dw.com/p/4X13U
Türkei Ankara | Anschlag in der Nähe des Innenministeriums
Picha: Cagla Gurdogan/REUTERS

Saa chache kabla ya  Bunge la Uturuki kuanza tena vikao vyake baada ya miezi mitatu ya mapumziko, mshambuliaji wa kujitoa mhanga amejilipua karibu na eneo lenye majengo ya bunge na ofisi nyingi za serikali kwenye mji mkuu wa Ankara.

Eneo lililoshambuliwa karibu na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Uturuki
Eneo lililoshambuliwa karibu na Wizara ya Mambo ya Ndani ya UturukiPicha: Cagla Gurdogan/REUTERS

Waziri wa Mambo ya Ndani wa Uturuki Ali Yerlikaya amesema shambulio hilo limewahusisha watu wawili mbele ya majengo ya wizara ya mambo ya ndani jijini Ankara, na ameongeza kusema kuwa mmoja wa washambuliaji hao  alikufa kwenye mlipuko huo na mwingine alikabiliwa na maafisa wa usalama.

Maafisa wawili wa polisi wamejeruhiwa kidogo kwenye shambulio hilo. Maafisa hao wawili wa polisi wanatibiwa hospitalini na hawako katika hali mbaya, kulingana na ripoti za vyombo vya habari.

Rais wa Uturki Recep Tayyip Erdogan
Rais wa Uturki Recep Tayyip ErdoganPicha: Mustafa Kamaci/AA/picture alliance

Waziri wa mambo ya ndani wa Uturuki, Ali Yerlikaya hakutoa taarifa za mara moja iwapo mashambulio hayo yanawahusisha wapiganaji wa Kikurdi au makundi ya wapiganaji wanaoegemea mrengo mkali wa kushoto au kundi la linalojiita Dola la Kiislamu IS ambalo limehusika na mashambulio mabaya kote nchini Uturuki hapo awali.

Waziri Yerlikaya amesema washambuliaji walifika katika eneo la tukio wakiwa ndani ya gari dogo la biashara.

Vikosi vya usalama kazini katika eneo karibu na wizara ya Mambo ya Ndani jijini Ankara
Vikosi vya usalama kazini katika eneo karibu na wizara ya Mambo ya Ndani jijini AnkaraPicha: Adem Altan/AFP/Getty Images

Picha za televisheni zilionyesha vikosi vya kutegua mabomu vikifanya kazi karibu na mahala ambako gari hilo liliegeshwa katika eneo ambalo liko karibu na Bunge Kuu la Uturuki na majengo mengine ya serikali.

Polisi wamezifunga njia zinazoelekea katikati ya jiji ya Ankara.

Soma pia:Erdogan: Uturuki inaweza kusitisha juhudi za kujiunga na EU

Mashambulio ya kujitoa mhanaga yamefanyika katika jiji la Ankara baada ya mengine kama hayo kufanyika mika kadhaa iliyopita.

Mwaka mmoja uliopita mshambuliaji wa kujitoa mhanga alijilipua kwenye mji wa Istanbul ambpo bwatu sita waliuawa na  wengine 81 walijeruhiwa. Mshambuliaji huyo alijilipua kwenye eneo lenye shughuli nyingi katikati mwa huo wa Istanbul mnamo Novemba 13, 2022.

Eneo la tukio limedhibitiwa
Eneo la tukio limedhibitiwaPicha: Cagla Gurdogan/REUTERS

Bunge la Uturuki lilipangwa kufunguliwa tena baada ya mapumziko ya miezi mitatu katika msimu wa kiangazi hii leo Jumapili 01/10/2023 na rais wa uturuki Recep Tayyip Erdogan.

Vyanzo:AP/RTRE

Mhariri: Chilumba Rashid