1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mkasa wa mwandishi habari Jamal Khashoggi

8 Oktoba 2018

Maafisa wa Uturuki wamedai kuwa mwandishi habari wa Saudi Arabia, Jamal Khashoggi, ameuliwa wakati alipokuwamo kwenye ubalozi mdogo wa Saudi Arabia mjini Istanbul lakini Saudi Arabia imezikanusha tuhuma hizo

https://p.dw.com/p/36Bar
Dschamal Chaschukdschi
Picha: Getty Images/AFP/M. Al-Shaikh

Uturuki imemwita balozi wa Saudia nchini humo ili kumtaka atoe ushirikiano kamili katika uchunguzi kuhusu kutoweka kwa mwandishi habari huyo ambaye Uturuki inasema aliuawa wakati alipoutembelea Ubalozi wa Saudi Arabia mjini Istanbul.

Maafisa wa Uturuki wameliambia  shirika la habari la Reuters kwamba, wanaamini kuwa mwandishi habari Khashoggi aliuliwa ndani ya ubalozi mdogo  wa Saudi Arabia. Shirika la habari la serikali la Uturuki limekariri taarifa ya polisi inayodai kwamba raia 15 wa Saudi Arabia waliwasili mjini Istanbul kwa kutumia ndege mbili na kwamba walikuwamo ndani ya ubalozi, siku ambapo mwandishi Khashoggi aliripotiwa kutoweka.

Waandishi habari na wanaharakati leo walikusanyika mbele ya ubalozi wa Saudi Arabia kwa lengo  la kutaka kupata habari juu ya kilichomfikaa  mwandishi  huyo. Watu hao wamesema wanataka kujua hasa kilichotokea kwa Khashoggi na mazingira ya kutoweka kwake. Muasisi wa shirika linalotoa ushauri kuhusu migogoro Mohamed Okda amesema wanataka kujua kilichotokea na wamesisitiza kwamba wote waliohusika wafikishwe mbele ya sheria. Wamesema wanahitaji majina ya watu ambao wamehusika katika kutoweka kwake, raia hao wa Saudi Arabia 15 waliokuja nchini Uturuki kumchukua au kumwua.Taarifa zaidi zinafahamisha kwamba balozi wa Saudi Arabia alikutana na naibu waziri wa mambo ya nje wa Uturuki Sedat Onal. Shirika moja binafsi la Televisheni nchini Uturuki limeripoti kwamba serikali ya Uturuki imetoa maombi kwa Saudi Arabia ili maafisa wa Uturuki wafanye uchunguzi kwenye jengo la ubalozi wa nchi hiyo mjini Istanbul.

Kushoto: Mchumba wa mwandishi aliyetoweka Jamal Kashoggi
Kushoto: Mchumba wa mwandishi aliyetoweka Jamal Kashoggi Picha: Getty Images/AFP/O. Kose

Mwandishi habari huyo Khashoggi ambae ni mpinzani wa utawala wa kifalme wa Saudi Arabia hakuonekana tena tangu alipoingia kwenye ubalozi mdogo wa nchi hiyo mjini Istanbul jumanne iliyopita. Kwa mujibu wa  taarifa, Kashoggi alikwenda kwenye ubalozi huo kwa ajili ya kuwasilisha hati za kumwezesha kumuoa mchumba wake wa kituruki.

Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan
Rais wa Uturuki Recep Tayyip ErdoganPicha: picture-alliance/abaca

Maafisa  wa  Uturuki  wanadai kwamba  mwandishi huyo anaeliandikia gazetia la Marekani la Washington Post aliuliwa ndani  ya ubalozi huo wa Saudi Arabia na mwili wake uliondolewa kutoka kwenye jengo la ubalozi lakini maafisa wa Saudi Arabia wamekanusha madai hayo na wamesema kuwa hayana  msingi. Rais wa Uturuki Recep Tayyip  Erdogan amesema anasuburi matokeo ya uchunguzi wa mkasa wa mwandishi huyo wa habari.

Ubalozi wa Saudi Arabia umesisitiza kwamba mwandishi huyo aliondoka baada ya kuwamo ndani ya jengo la ubalozi huo, kinyume na madai yanayotolewa na maafisa wa Uturuki. Mwandishi huyo wa Saudi Arabia  Jamal Khashoggi aliamua kukimbilia Marekani mwaka mzima uliopita baada ya kukimbia Saudi  Arabia wakati  ambapo serikali ya kifalme ya nchi hiyo ilipoanzisha msako dhidi ya wasomi na wanaharakati waliokuwa wanakosoa sera za mritihi wa mfalme Mohammed bin Salman.

Mwandishi:Zainab Aziz/AP/RTRE

Mhariri: Iddi Ssessanga