1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MigogoroUlaya

Urusi: Ukraine kujiunga na NATO ni tangazo rasmi la vita

Hawa Bihoga
17 Julai 2024

Rais wa zamani wa Urusi Dmitrz Medvedev amesema kujiunga kwa Ukraine katika jumuiya ya NATO itakuwa ni tangazo la vita dhidi ya Moscow na "busara" ya muungano huo ni kutoipokea kunaweza kuzuia sayari kusambaratika.

https://p.dw.com/p/4iPNU
Urusi | Dmitry Medwede akilakiwa na mwanajeshi wa Urusi eneo la shughuli za kijeshi.
Rais wa zamani na Mwenyekiti wa Baraza la Usalama Urusi akitembelea mazoezi ya wanajeshi wa Urusi.Picha: ASSOCIATED PRESS/picture alliance

Kauli za Medvedev inafuatia viongozi wa jumuiya NATO kuahidi juma lililopita katika mkutano wao wa kilele kwamba wataendelea kuiunga mkono Ukraine kikamilifu bila kuyumba.

Viongozi hao ambao wamekuwa wakionesha mshikamano kwa Ukraine tangu uvamizi wa Urusi alisema kwamba uungaji mkono wao ni pamoja na uanachama Kyiv kwa NATO, lakini hawakusema wazi ni lini hasa Kyiv itakuwa mwanachama kamili wa jumuiya hiyo ya NATO.

Rais huyo wa zamani wa Urusi ambae kwa sasa ni mwenyekiti wa Baraza la Usalama Urusi na mashauri wa karibu wa ikulu ya Kremlin alikiambia chombo kimoja cha habari kuwa uanachama wa Ukraine utavuka kitisho cha moja kwa moja cha usalama wa Moscow.

Katika mazungumzo yake yaliochapishwa leo Jumatano Medvedev aliongeza kwamba wapinzani wa Urusi wamekuwa wakichukua hatua dhidi ya Msocow kwa miaka chungumzima, ikiwemo kutanua muungano wao kwa namna ambayo haiwezi kuzuilika na kusisitiza kwamba Urusi haitishii NATO bali itajibu majaribio ya muungano huo ili kulinda na kuendeleza maslahi yake.

Soma pia:Medvedev asema Moscow italipa kisasi kwa vikwazo vya magharibi

Medvedev, ambaye wakati wa urais wake mnamo 2008-2012 alichukuliwa kama mwanaharakati wa kisiasa wa Magharibi, ameionya Marekani na washirika wake kuendelea kuipatia Ukraine silaha kunaweza kusababisha janga kubwa la nyuklia.

Ukraine: Idadi kubwa ya watu hawajulikani walipo

Nako nchini Ukraine Wizara ya Mambo ya Ndani imesema takriban watu 42,000 hawajulikani walipo idadi ambayo inajumuisha raia pamoja na wanajeshi.

Afisa katika wizara hiyo anaeongoza kitengo cha watu waliopotea Dmytro Bohatiuk alisema kwamba idadi hiyo ilifikia watu 51,000.

Aidha idadi ya waliopotea ilipungua baada ya maelfu ya wafungwa wa kivita kuhesabiwa.

Baadhi ya Waukraine waamua kutoroka kuliko kupigana na Urusi

Dmytro alisema kwamba changamoto nyingine ambayo inaikabili idara hizo ni pamoja na kutotambuliwa kwa miili ya watu waliouwawa kwenye uwanja wa vita na wizara za Ulinzi nchini humo haikusanyi sampuli za vinasaba kutoka kwa waathirika.

Australia: Urusi ilihusika kudungua ndege ya Malaysia

Maafisa, ndugu na jamaa wa abiria waliofariki wakati Ndege ya Malaysia iliodunguliwa katika anga la Ukraine wamekusanyika katika Bunge la Australia leo siku ya Jumatano kuadhimisha miaka 10 ya mkasa huo.

Waziri wa mambo za nje wa Australia Penny Wong amesema, matokeo ya mahakama yanaonesha Urusi imehusika katika kudungua ndege hiyo MH17

"Hivyo wakati tumeshutshwa kwamba Urusi imejiondoa kaika hatua iliyoanzishwa na Australia na Uholanzi katika Shirika la Kimataifa la Usafiri wa Anga, kesi itaendelea, na hatutazuiliwa katika ahadi yetu ya kuiwajibisha Urusi." Alisema Waziri Wong.

Soma pia:Malaysia yasema itaendelea kuitafuta ndege MH370

Ndege hiyo aina ya Boeing 777 ilikuwa ikitoka Amsterdam kuelekea Kuala Lumpur mnamo Julai 17, 2014, wakati wa mzozo kati ya wanaounga mkono Urusi kujitenga na vikosi vya Ukraine.