1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Tshisekedi aongoza matokeo ya awali uchagzi DR Kongo

26 Desemba 2023

Tume ya Uchaguzi nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, CENI, imetoa matokeo zaidi ya awali ya uchaguzi wa rais, yakionesha rais Felix Tshisekedi anaongoza kwa mbali, akifuatiwa na mfanyabiashara Moise Katumbi.

https://p.dw.com/p/4aZf8
Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo | Rais Felix Tshisekedi
Matokeo ya awali yanaonyesha Rais Tshisekedi anaongoza kwa asilimia 81.Picha: AFP

Matokeo yaliyotangazwa na CENI kufikia sasa yanatokana na takriban kura milioni 1.9, kati ya jumla ya wapiga kura milioni 44 waliojiandikisha katika nchi hiyo kubwa ya Afrika ya kati yenye ukubwa sawa na eneo la Ulaya Magharibi na yenye wakazi zaidi ya milioni 100.

Ceni alisema Tshisekedi mwenye umri wa miaka 60, aliye madarakani tangu 2019 na anayewania muhula wa pili wa miaka mitano, alikuwa anaongoza kwa zaidi ya asilimia 81 ya kura.

Soma pai: Wagombea wa upinzani nchini Kongo wapanga kufanya maandamano kupinga zoezi la uchaguzi wa rais

Alikuwa akifuatiwa kwa mbali na mfanyabiashara tajiri na gavana wa zamani wa jimbo la Katanga Moise Katumbi, 58, akiwa na zaidi ya asilimia 15 ya kura na mtendaji mkuu wa zamani wa mafuta Martin Fayulu, 67, kwa zaidi ya asilimia moja.

DR Kongo Kinshasa CENI Tume ya Uchaguzi
Makao makuu ya tume ya uchaguzi, CENI, mjini Kinshasa.Picha: Dirke Köpp/DW

Wapinzani wengine karibu 20, akiwemo Denis Mukwege, mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel mwenye umri wa miaka 68, walishindwa kupata asilimia moja.

Ceni haijatangaza idadi ya watu waliojitokeza kupiga kura katika uchaguzi wa Desemba 20 na 21 lakini bado imekuwa ikitoa matokeo hatua kwa hatua tangu Ijumaa, ambayo ni pamoja na uchaguzi wa wabunge, mikoa na mitaa.

Miito ya utulivu na kujiepusha na vurugu

Uchaguzi huo ulipaswa kufanyika siku ya Jumatano pekee lakini uliongezewa siku kwa sababu ya changamotokadhaa za usambazaji wa vifaa vya kupigia kura. Wagombea wa upinzani walilaani "machafuko" na "makosa" ambayo walidai yaliharibu kura.

Baadhi wanapanga maandamano Jumatano ijayo, huku wengine wakitaka uchaguzi huo kufutwa moja kwa moja.

Uchaguzi DRC 2023: Matokeo ya awali yasubiriwa

Askofu Mkuu wa Kanisa Katoliki la Kinshasa, Kadinali Fridolin Ambongo, aliutaja uchaguzi huo kuwa "vurugu kubwa" wakati wa misa yake ya Krismasi siku ya Jumapili.

Kama ilivyokuwa kwa balozi zaidi ya kumi zilizotoa matamko kabla yake, kadinali huyo alitoa wito wa "tahadhari na kujizuia", katika nchi hiyo maskini lakini tajiria wa madini na historia ndefu ya utawala wa kimabavu na migogoro.

Soma pia: Chama cha FCC chadai Tshisekedi ameuvuruga uchaguzi wa Kongo

Mbali na mashaka ya wapinzani kuhusu mchakato wa uchaguzi huo, kampeni yake ilikumbwa na mzozo wa mashariki mwa nchi hiyo, ambayo imeshuhudia ongezeko kubwa la mvutano katika kipindi cha miaka miwili iliyopita kutokana na kuibuka tena kwa waasi wa M23 wanaodaiwa kuungwa mkono na Rwanda.

Kigali inakanusha madai hayo.