1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Mataifa tajiri kuipa Afrika fedha kukabiliana na tabianchi

6 Septemba 2022

Mataifa Tajiri yamesema yatatumia karibu dola bilioni 25 ifikapo mwaka wa 2025 ili kupiga jeki juhudi za Afrika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Mkutano wa kilele wa tabia nchi ulifanyika Rotterdam, Uholanzi

https://p.dw.com/p/4GSAN
Niederlande Africa Adaptation Summit in Rotterdam
Picha: ANP/IMAGO

Mkutano huo wa kilele ulikuwa wa kwanza kabisa kuwahi kuwaleta pamoja viongozi kutoka serikali nyingi na taasisi, kama vile Shirika la Biashara Ulimwenguni – WTO na Shirika la Kimataifa la Fedha – IMF, kujadili mbinu za kukabiliana na tabia nchi barani Afrika. Kiasi cha fedha kilichoahidiwa kilielezwa kuwa kikubwa zaidi kuwahi kutolewa duniani katika juhudi za kukabiliana na tabia nchi.

Soma pia: Umoja wa Mataifa wasema mawimbi ya joto kali yatajitokeza mara kwa mara hadi 2060

Hata hivyo, viongozi wa Afrika waliohudhuria wamekosoa kutokuwepo kwa wenzao wa nchi za Magharibi katika mkutano huo. Rais wa Senegal na ambaye ni mkuu wa Umoja wa Afrika Macky Sall na mwenzake wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo Felix Tshisekedi walisema nchi tajiri zinazochangia pakubwa katika uzalishaji wa gesi ya kaboni zilipaswa kushiriki. "Sote tunaishi katika sayari hii ya dunia na wale ambao wanachangia ongezeko la joto - na hii imethibitishwa kisayansi - ni nchi zilizoendelea kiviwanda, kwa hiyo Ulaya, hasa Marekani, China na kadhalika. Zinahusika na uchafuzi na ongezeko la joto duniani."

Akinwumi Adesina Porträt Entwicklungsbank Afrika
Akiwunmi Adesina, Rais wa Benki ya Maendeleo AfrikaPicha: Getty Images/S. Gallup

Waziri Mkuu wa Uholanzi Mark Rutte ndiye kiongozi pekee wa Magharibi aliyehudhuria.

Akinwumi Adesina, rais wa Benki ya Maendeleo ya Afrika – ADB ameuambia mkutano huo kuwa Afrika sio tu imeathirika na mabadiliko ya tabia nchi, bali pia imeteseka na hali hiyo. "Benki ya Maendeleo ya Afrika iliweka dola bilioni 12.5 kati ya dola bilioni 25. Kwa hivyo sisi sio ombaomba. Siyo? Tunasema kuwa hatukusababisha tatizo. Tunakuja kwenye mazungumzo na roho safi, dhamira nzuri kabisa. Tukutane katikati."

Afrika na mzozo wa tabia nchi

Afrika ndilo bara lililopo katika hatari kubwa zaidi ya tabianchi ulimwenguni, kwa mujibu wa tathmimni ya karibuni ya Umoja wa Mataifa. Mkutano huo wa kilele ni muhimu kwa sababu umefanyika kabla ya mkutano wa kilele wa 27 wa COP27 utakaofanyika nchini Misri, Novemba. 

Soma pia: Mkutano wa hali ya hewa wa Petersberg nchini Ujerumani

Dürre in Uganda
Afrika inakabiliwa na athari za mabadiliko ya tabianchiPicha: Badru Katumba/AFP/Getty Images

Mkutano wa Kilele wa Afrika unafanyika ikiwa ni chache tu baada ya Shirika la Ushirikiano wa Kiuchumi na Maendeleo – OECD kugundua kuwa nchi Tajiri zimeshindwa kutimiza ahadi zao za mwaka wa 2009 za kutumia dola bilioni 100 kwa mwaka ifikapo 2020 ili kuzisaidia nchi zinazoendelea kukabiliana na kuongezeka kwa joto duniani. Adesina ameongeza kuwa Afrika hupoteza karibu kati ya dola bilioni 7 na dola bilioni 15 kwa mwaka kutokana na mabadiliko ya tabia nchi.

Soma pia: Moto wa msituni wazusha sokomoko kusini mwa Ulaya

Vipi Afrika inaweza kupambana na mabadiliko ya tabia nchi?

Adesina ameuambia mkutano huo wa kilele kuwa Afrika haina raslimali za kifedha kupambana na mabadiliko ya tabia nchi kwa sababu inapokea tu asilimia 3 ya jumla ya ufadhili wa mazingira. Amesema Afrika itahitaji kati ya dola trilioni 1.3 na dola trilioni 1.6 ili kutekeleza ahadi zake kwa makubaliano ya Paris, ikiwa ni gharama ya kati ya dola bilioni 140 na dola bilioni 300 kwa mwaka. Mkuu huyo wa benki ya Maendeleo ya Afrika ameiambia DW kuwa mataifa ya Afrika yana hifadhi kubwa za gesi na kutokana na mzozo wa Ulaya, yanaweza hata kuzisaidia nchi za Ulaya kupata gesi katika siku za usoni.

https://www.dw.com/en/africa-rich-nations-pledge-funds-at-climate-crisis-summit/a-63026384