1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW
MichezoBrazil

Mashindano mapya ya vilabu kufanyika sambamba na CONCACAF

15 Julai 2023

Mashindano mapya ya Kombe la Dunia la FIFA ngazi ya klabu ambayo yatafanyika nchini Marekani mwaka 2025, yanaweza kufanyika sambamba na mashindano ya Kombe la CONCACAF ambayo pia yanaandaliwa huko Marekani.

https://p.dw.com/p/4TwMZ
FIFA Klub-Weltmeisterschaft | Sieger Real Madrid
Wachezaji wa Real Madrid wakinyajua Kombe la Dunia la FIFA ngazi ya klabu baada ya kuifunga Al Hilal katika uwanja wa Abdellah, Rabat.Picha: 900/Cordon Press/picture alliance

Mashindano mapya ya Kombe la Dunia la FIFA ngazi ya klabu, ambayo yatafanyika nchini Marekani mwaka 2025, yanaweza kufanyika sambamba na mashindano ya Kombe la shirikisho la soka la mataifa ya Marekani ya Kaskazini, Kati na Visiwa vya Carribean CONCACAF ambayo pia yanaandaliwa huko Marekani.

Rais wa CONCACAF Victor Montagliani ambaye pia ni makamu wa rais wa FIFA, ameliambia shirika la habari la AFP kwamba mazungumzo tayari yanaendelea kati ya mashirikisho hayo mawili ya soka ili kuepusha migongano ya nyakati za kuanza kwa mechi.

Soma pia: Brazil yamtangaza Carlo Ancelotti kuwa kocha mkuu wa timu ya taifa kuanzia mwaka 2024

FIFA ilitangaza mwezi uliopita kwamba mashindano ya Kombe la Dunia la FIFA ngazi ya klabu yenye muonekano mpya na ambayo yamepanuliwa na kushirikisha vilabu 32, yataanza nchini Marekani mnamo mwaka 2025.

CONCACAF huandaliwa kila baada ya miaka miwili

Fußball | Champions League FInale | Manchester City vs Inter Mailand
Kocha wa Manchester City Pep Guardiola akitoa maelekezo kwa wachezaji wake katika mchezo wa fainali dhidi ya Inter Milan.Picha: MIke Egerton/PA Wire/picture alliance

Mashindano ya Kombe la Dhahabu la CONCACAF huandaliwa kila baada ya miaka miwili na mechi ya fainali huchezwa siku ya Jumapili mjini Los Angeles.

"Tayari tumeingia kwenye majadiliano na FIFA, na timu zote zitakazoshiriki mashindano hayo, ili kuhakikisha kuna utaratibu mzuri wa maandalizi hadi kuelekea mechi. Hali hiyo itakuwa ushindi pia kwa mashabiki," Montagliani amesema.

"Kunaweza kukatokea mwingiliano. Lakini nyakati hazitofanana kama ilivyotokea siku za nyuma katika mashindano yaliyopita. Lakini nadhani mwingiliano ni sawa," ameongeza makamu huyo wa rais wa FIFA.

Soma pia: Euro 2022 kwa wanawake yatinga nusu fainali 

Viwanja huenda visiwe tatizo kwa ajili ya mashindano hayo kwani tayari viwanja vya mchezo wa soka wa Marekani NFL pamoja na viwanja vinavyotumika kuandaa mechi za ligi kuu ya soka nchini humo MLS vimewahi kutumika kwa ajili ya kuandaa mechi za kimataifa.

Tofauti ya nyakati kati ya majimbo ya pwani ya Mashariki na Magharibi ya Marekani pia inaweza kusaidia kupunguza mzozo kati ya mashindano hayo mawili, japo kunaweza kuibuka suala la upatikanaji wa wachezaji.

Montagliani amesema kutolewa kwa ruhusa ya siku za mapumziko kwa kila mashindano kunaweza kupunguza kusuluhisha suala hilo la upatikanaji wa wachezaji.

Afrika kuwakilishwa na timu nne

Fußball I  Victor Osimhen - Nigeria
Mchezaji wa timu ya taifa ya Nigeria Victor Osimhen katika pambano dhidi ya Sierra Leone.Picha: Simone Scusa/Shengolpixs/IMAGO

"Kunaweza kuwa na mwingiliano katika hatua ya makundi. Lazima tuhakikishe nyakati za kuanza kwa mechi zimepangwa vizuri. Ukifanya sawa, ratiba itakwenda vizuri. Ni juu yetu na FIFA kuhakikisha kwamba kila kitu kinakwenda vizuri na timu zetu zishirikiane. Tayari tuko kwenye majadiliano."

Ingawa nafasi nyingi za kufuzu kwa mashindano hayo bado hazijaamuliwa, Kombe la Dunia la FIFA ngazi ya klabu, litajumuisha vilabu kama vile Real Madrid, Manchester City, Chelsea, Flamengo, Palmeiras, Leon ya kutoka Mexico na Seattle Sounders inayoshiriki ligi kuu ya kandanda ya Marekani MLS.

FIFA iliamua mwezi Februari kuwa mashindano hayo mapya yatajumuisha timu 12 kutoka Ulaya, 6 kutoka Amerika ya Kusini na bara Asia, Africa na CONCACAF zitaziwakilisha na timu nne kutoka kila eneo.

FIFA imeanzisha uendeshaji wa shughuli zake na tayari ina ofisi Miami na hivi karibuni ilitia saini makubaliano ya kushirikiana na CONCACAF juu ya mashindano ya kikanda kama vile Kombe la Dhahabu na Ligi ya Mataifa ya Ulaya.