1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marsabit yasitisha uhasama

15 Novemba 2022

Tume ya Uwiano na Utangamano ya Kenya (NCIC) imefungua ofisi ya kwanza ya upatanishi jimboni Marsabit ambako inasema imeridhishwa na hatua za kusitisha uhasama huku mchakato wa kuwafidia waathirika zikiendelea.

https://p.dw.com/p/4JXQk
Kenia Dürre l Kadaver einer Kuh, im Hintergrund Turkana-Frauen mit Feuerholz
Picha: Simon Maina/AFP

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa kituo hicho, Mwenyekiti wa NCIC, Samuel Kobia, alisema majadiliano yanaendelea kuhusu namna ya kuwasaidia walioathirika na vurugu hizo kama sehemu ya kusuluhisha mizozo. Kobia alisema ni kupitia hatua hizo ambapo waliofurushwa makwao watarejea na kuanza kujenga upya maisha yao

“Huu ni wakati ambapo wakaazi wanahitaji msaada zaidi. Kuna mahitaji ya chakula, kuwajengea nyumba walioathirika, kuwapa ushauri nasaha na upatinisho. Kama haya yatawezekana, basi kuna uwezekano kukawa na amani ya kudumu.” Aliongeza Kobia.

Umoja wa Ulaya wasaidia ukame

Kenia Marsabit Dürre Tierkadaver
Mizoga ya wanyama kutokana na ukame Marsabit kaskazini mashariki mwa Kenya.Picha: Michael Kwena/DW

Kwa upande wake, Balozi wa Umoja wa Ulaya nchini Kenya, Henriette Geiger, alitajaukameunaoshuhudiwa nchini humo kama chachu ya mizozo katika jamii za wafugaji.

Balozi huyo alisema Umoja wa Ulaya tayari umetumia euro milioni 400 kuwasaidia wakaazi katika majimbo yaliyoathirika na ukame katika kipindi cha miaka mitano iliyopita.

"Mwaka huu tumewekeza euro milioni 62 katika majimbo kame kuwasaidia wakaazi kwenye masuala ya ukame. Lakini fedha bado hazitoshi kabisa."

Kenya yaanza kusambaza chakula kwa wahanga wa ukame jimboni Marsabit

Mbunge anayewakilisha wanawake kutoka Marsabit, Naomi Jillo, aliyalaumu mashirika ya kijamii yanazofanya kazi jimboni humo kwa kuchangia uhasama kwa kile alichodai kuwa hakuna usawa katika ugavi wa misaada ya kiutu.

Ubaguzi watajwa

Afrika Nahrungsmittelspende Church World Service Organisation in Marsabit
Mgawo wa chakula kwa waathirika wa ukame jimboni Marsabit.Picha: Michael Kwena/DW

Jillo alidai kuwa mizozo imekuwa ikiibuka kutokana na hatua za mashirika hayo kuendelea kuyasahau maeneo mengine ya kaunti.

"Wakati hamtoi huduma sawa kwa jamii zote hapa Marsabit, mnazua uhasama baina yao. Tafadhalini toeni huduma kwa usawa kwa sababu kiangazi kinachoshuhudiwa kule Moyale ndicho kile kile kinashuhudiwa kule Maikona." Alisema.

Katika kipindi cha miaka tano iliyopita, watu wasiopungua 400 wameuawa kutokana na machafuko ya kikabila huku upatanishi ukiendelea kuzituliza jamii zilizowapoteza jamaa zao kama sehemu ya kupata mwafaka wa kudumu.

Shuguli za upatanishi jimboni hapa pia zinapigwa jeki na serikali ya Uswisi pamoja na shirika la kimatiafa la amani la Interpeace.

Imeandikwa na Michael Kwena/DW Marsabit