1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Marekani yawaomba washirika wa NATO kuungana dhidi ya China

25 Machi 2021

Waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Anthony Blinken ameufungua mkutano na washirika wa jumuiya ya kujihami ya NATO kwa kuwaoma wanachama wenzake kushirikiana nayo dhidi ya kitisho cha China.

https://p.dw.com/p/3r5PD
Belgien Brüssel | NATO Treffen der Außenminister - Antony Blinken
Picha: Virginia Mayo/REUTERS

Waziri wa mambo ya kigeni wa Marekani Anthony Blinken jana ametoa hotuba ya ufunguzi katika siku ya pili ya mikutano na washirika wa Jumuiya ya Kujihami ya NATO, akigusia masuala yahusuyo mahusiano ya Marekani na washirika wake, vitisho vya Urusi hadi China pamoja na changamoto za kiulimwengu. 

Kwenye hotuba hiyo, Blinken alijizuia kutoa maneno makali ya kuikosoa China na badala yake alitoa mwito kwa washirika wake kuungana na Marekani.

Blinken, alirudia msimamo wa Marekani wa kuiunga mkono NATO, akisema nchi hiyo imejitolea kikamilifu, ikiwa ni pamoja na kutekeleza kifungu cha 5, kinachoelezea wajibu wa kuhakikisha ulinzi miongoni mwa wanachama.

Soma Zaidi: NATO, EU wamwalika Biden kujenga upya uhusiano na Marekani

Lakini serikali kadhaa za Marekani zilizopita zilisisitiza kuhusu michango, zikiwataka wanachama wengine wa NATO kuongeza mchango wa ulinzi kwenye jumuiya hiyo kwa asilimia 2 ya pato lao jumla la ndani.

Blinken pia amehimiza kuyapa kipaumbele maamuzi yahusuyo vitisho vya kiulimwengu kama janga la COVID-19 na mabadiliko ya tabianchi.

Türkei Protest gegen Uiguren-Politik in China
China inakosolewa vikali kukiuka haki za binaadamu dhidi ya Waislamu walio wachache wa Uighur, katika jimbo la XijiangPicha: Getty Images/AFP/O. Kose

Ukosoaji dhidi ya China

Kwenye hotuba hiyo Blinken ameikosoa kile alichoita tabia ya uonevu ya China huku akiapa kuishinda. Hata hivyo amesema hiyo haimaanishi kwamba mataifa mengine hayapaswi kushirikiana na China pale inapotakikana, kwa mfano kwenye changamoto za mabadiliko ya tabianchi na usalama wa kiafya.

Alisema "Marekani haitawalazimisha washirika wetu kuchagua ama sisi au wao. Hakuna mjadala kuhusiana na mwenendo wa Beijing kwamba unatishia muungano wetu wa kiusalama pamoja na ustawi na kwamba inafanya kileliwezekanalo kukiuka misingi ya mifumo ya kisheria ya kimataifa na maadili yetu. Lakini hiyo haimaanishi kwamba nchi haziwezi kushirikiana na China pale inapowezekana kwa mfano katika changamoto kama mabadiliko ya tabianchi na usalama wa kiafya."

Wasiwasi baina ya China na magharibi umeongezeka hivi karibuni baada ya Umoja wa Ulaya, Marekani, Canada na Uingereza kuwawekea vikwazo maafisa wa China na makampuni kufuatia madai ya ukiukwaji wa haki za binaadamu, hatua ambayo pia ilijibiwa na China kwa vikwazo. 

Belgien Brüssel | NATO Treffen der Außenminister - Antony Blinken
Marekani na Ulaya wamekubaliana kushirikiana katika masuala kadhaa, hususan vitisho vinavyoibuliwa na China na UrusiPicha: Olivier Hoslet/AFP/Getty Images

Blinken pia aligusia tabia ya ubabe ya Urusi, akisema anadhani ni vyema wakaanzisha mahusiano na taifa hilo ambayo yanaweza kutabirika na endelevu. Hata hivyo alisema pamoja na hatua hiyo, bado hawatasita kuiwajibisha Urusi kutokana na hatua zake za hovyo na za ushindani ama uadui. Kabla ya hotuba hiyo, NATO ilikosoa vikali sera za ndani na za nje za Urusi.

Umoja wa Ulaya na Marekani wakubali kushirikiana.

Baada ya hotuba hiyo, Blinken na Mkuu wa sera za nje wa Umoja wa Ulaya Josep Borrell walitoa taarifa ya pamoja, wakieleza kukubaliana kuanzisha upya mazungumzo ya pamoja kuhusu China na Urusi. Walijadiliana pia kuhusu changamoto za mabadiliko ya tabianchi, chanjo ya corona, Iran na Uturuki.

Suala la kuongezeka kwa ushawishi wa China katika siasa za ulimwengu, linatarajiwa kuwa ajenda muhimu katika mkutano wa wakuu wa mataifa wanachama wa NATO, baadae mwezi Juni.

Soma Zaidi: Marekani na Japan kuijadili China

Mashirika: DW